MKOA WA LINDI YAAGIZWA KUSITISHA UMWAGAJI WA MAJI TAKA DAMPO - THE HABARII

ASAS GROUP

Habari Mpya


Monday 25 February 2019

MKOA WA LINDI YAAGIZWA KUSITISHA UMWAGAJI WA MAJI TAKA DAMPO

Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira Mhe. Mussa Sima akipata maelezo kutoka kwa Mkuu wa Wilaya ya Lindi Bw. Shaibu Ndemanga mara baaya ya kufanya ziara ya kukagua dampo la Manispaa hiyo ili kujionea uzingatiaji wa Sheria ya Mazingira. Katika dampo hilo lilipo eneo la Machole Manispaa ya Lindi Naibu Waziri Sima ameuagiza uongozi wa Mkoa kusitisha umwagaji wa maji taka katika eneo hilo.

Na Lulu Mussa, LINDI 

 NAIBU Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira Mhe. Mussa Sima ameuagiza Uongozi wa Mkoa wa Lindi kusitisha mara moja hatua ya kumwaga maji taka katika dampo la Halmashauri hiyo.

Agizo hilo limetolewa hii leo Mkoani Lindi mara baada ya kufanya ziara ya kikazi ya kukagua uzingatiaji na Usimaimizi wa Sheria ya Mazingira ya Mwaka 2004. Akiwa katika Halmashauri hiyo Mhe. Sima amejione uchafuzi mkubwa mazingira kwa Halmashauri ya Lindi kuchanganya taka ngumu na maji taka katika dampo moja na kuagiza uongozi wa Mkoa huo kusitisha mara moja utaratibu huo na kupiga marufuku wananchi kuingia kiholela katika dampo hilo.

 “Utaratibu wa kutofautisha taka uanzie nyumbani na katika sehemu za kukusanyia taka, taka zikiletwa hapa dampo ziwe zimeshachambuliwa, huu utaratibu wa watu kuingia hapa dampo kuokota chupa za plastiki usitishwe mara moja” Alisisitiza Naibu Waziri Sima.

 Waziri Sima amesema kuwa kuna uwezekano mkubwa wa taka hatarishi kutupwa dampo kwakuwa hakuna mkakati madhubuti wa kutenganisha taka hizo toka kwenye vyanzo vya uzalishaji.

 Ikiwa ni siku ya kwanza ya ziara yake katika Mkoa wa Lindi Naibu Waziri Sima pia amepata fursa ya kuongea na Viongozi mbalimbali wa Halmashauri ya Manispaa ya Lindi wakiwemo madiwani na viongozi wa Serikali za Mitaa kuweka mikakati madhubuti ya kutunza Ikolojia ya Vyanzo vya Maji ambavyo ni mto Njenje na Parang’andu ambavyo hutirisha maji yake katika Mto Luwengu ambao humwaga maji yake kati katika Mto Rufiji.

 “Ndugu zangu sote tunafahamu umuhimu wa hifadhi ya Mazingira na umuhimu wa Bonde la Mto Rufiji katika uzalishaji wa Umeme wa Uhakika, sisi watu wa Mazingira hii kwetu ni fursa, maana uzalishaji wa umeme utasaidia kuhifadhi mazingira kwa kupunguza matumizi ya kuni na mkaa.

Nawasihi wote tuwe mstari wa mbele katika kuhakikisha sisi tunakuwa mfano wa kulinda vyanzo vya maji.” Sima alisisitiza. Aidha, Naibu Waziri Sima pia amepata fursa ya kutembelea Hospitali ya Mkoa wa Lindi na kuridhishwa na Mtambo maalumu wa kuteketeza taka ulipo Hospitalini hapo na kuagiza majengo yayojengwa katika Sekta ya Afya kuweka miundombinu ya kuvuna maji.

 Naibu Waziri Sima yuko katika ziara ya kukagua changamoto za kimazingira pamoja na kuweka mikakati ya kuzipatia ufumbuzi na pia kuhimizi usimamizi endelevu wa Mazingira kwenye ikolojia ya vyanzo vya maji vinavyochangia maji katika Bonde la Rufiji.

No comments:

Post a Comment