FAMILIA ya Rais Mstaafu wa Awamu ya Tatu Hayati Benjamin William Mkapa hatimaye imeweka wazi ugonjwa uliomuua kiongozi huyo mstaafu wa taifa la Tanzania. Familia ya kiongozi huyo imeweka wazi taarifa hizo leo kwenye ibada takatifu maalumu ya Kanisa Katoliki ya kumuaga hayati Benjamin Mkapa iliyofanyika Uwanja wa Uhuru jijini Dar es Salaam.
Akizungumza leo katika Uwanja wa Uhuru, Msemaji wa familia ya Mkapa, William Erio alisema hayati Mkapa alianza kujisikia vibaya siku chache kabla ya kifo chake na baada ya kwenda hospitali na kupima alibainika ana maleria na kuanza matibabu huku akiwa amepumzishwa hospitalini.
Alisema baadaye alijisikia vizuri na kuendelea na matibabu akiwa hospitalini. Msemaji huyo anabainisha kuwa akiwa akiendelea na matibabu hospitalini alipatwa na mshtuko wa moyo ghafla na alipofanyiwa uchunguzi na madaktari walibaini alikuwa amepoteza maisha.
Aidha aliwataka Wananchi kuamini hicho ndicho kilichosababisha kifo cha kiongozi huyo na si vinginevyo, kama baadhi ya watu wasio na utu wamekuwa wakipotosha juu ya chanzo cha kifo cha kiongozi huyo.
Rais huyo Mstaafu wa Awamu ya Tatu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, alifariki dunia usiku wa kuamkia Julai 24 akipata matibabu jijini Dar es Salaam.
No comments:
Post a Comment