Mkurugenzi wa Usalama na Mazingira Wizara ya Ujenzi
Eng. Kashinde Musa akizungumza na wafanyakazi wa mizani kanda ya ziwa wakati
akifungua rasmi mafunzo ya siku tatu ya kuwajengea uwezo kufanya kazi kwa
weledi jijini Mwanza.
Baadhi ya watumishi wa mizani kutoka mikoa ya kanda
ya ziwa wakifuatilia mafunzo ya utendaji kazi wenye weledi kwa wafanyakazi wa
mizani wa mikoa sita ya kanda hiyo yanayoendelea jijini Mwanza.
Mkurugenzi wa Usalama na Mazingira Wizara ya Ujenzi
Eng. Kashinde Musa akisisitiza jambo wakati akizungumza na waandishi wa habari
mara baada ya kufua mafunzo kwa wafanyakazi wa mizani kanda ya ziwa
yanayoendelea jijini mwanza.
Mkurugenzi wa Usalama na
Mazingira Wizara ya Ujenzi Eng. Kashinde Musa amewaasa wafanyakazi wa mizani kujiepusha
na vitendo vya rushwa ili kulinda miundombiniu ya barabara na hivyo kufanya kazi
kwa tija.
Akizungumza jijini Mwanza
wakati akifungua mafunzo kwa wafanyakazi wapya wa mizani kanda ya ziwa Eng.
Kashinde amesema Serikali itaendelea kuchukua hatua kali za kisheria kwa wote
watakaobainika kujihusisha na rushwa kwa kuzidisha uzito na kusababisha
barabara kuharibika kabla ya wakati uliokusudiwa.
“Serikali imewaamini
na itawapa ushirikiano na mafunzo kila wakati ili mfanye kazi kwa weledi na
hivyo kuleta tija kwa miundombinu ya barabara na sekta ya usafirishaji kwa
ujumla”, amesema Eng. Kashinde.
Amesema Serikali
inaendelea kutenga fedha kwa ajili ya ujenzi wa miundombinu ya barabara mpya
kwa kiwango cha lami sambamba na kujenga mizani kwenye maeneo ya kimkakati ili
kudhibiti uharibifu unaotokana na uzidishaji uzito wa magari na kuhakikisha
barabara zinalindwa ili zidumu kwa kipindi kilichokusudiwa.
“Pasipo kudhibiti
uzito barabara zetu zitaharibika mapema na hivyo kusababisha Serikali kuingia
gharama kubwa za matengenezo, jambo ambalo lina athari katika kukuza uchumi wa
nchi”, amesisitiza Mkurugenzi huyo wa Usalama na Mazingira Wizara ya ujenzi.
Mafunzo hayo
yamewalenga wafanyakazi wapya wa mizani katika mikoa ya Mwanza, Shinyanga, Simiyu,
Mara, Geita, na Kagera lengo likiwa ni kupata uelewa wa pamoja katika
utekelezaji wa Sheria ya Udhibiti Uzito wa Magari ya Mwaka 2016 na Kanuni zake
za mwaka 2018, taratibu za utendaji kazi kwenye mizani, maadili ya Utumishi wa
Umma, elimu kuhusu vitendo vya rushwa na utoaji wa huduma bora kwa wateja.
Kwa upande wake Kaimu
Meneja wa mizani TANROADS makao makuu Eng. Japhet Kivuyo amesisitiza umuhimu wa
watumishi wa mizani kufanya kazi kwa weledi na ubunifu ili kuelimisha na
kutatua changamoto zinazowakabili wasafirishaji na hivyo kuwezesha sekta ya
usafirishaji nchini kuwa na tija.
“Hakikisheni mnatoa huduma
bora ili wasafirishaji wa ndani na nje ya nchi wawaelewe na wafuate sheria bila
shuruti na hivyo kulinda barabara zetu”, amesema Eng. Kivuyo.
Zoezi hilo la utoaji
elimu linalofanywa na Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS), ni endelevu
ambapo takriban wasafirishaji 2,100 katika miji na vijiji vyenye uzalishaji
mkubwa wa mizigo wamepata mafunzo hayo katika kipindi cha mwaka wa fedha wa
2022/2023 na 2023/2024.
No comments:
Post a Comment