UZINDUZI WA KAMPENI ZA CCM USHETU - THE HABARII

ASAS GROUP

Habari Mpya


Monday 27 September 2021

UZINDUZI WA KAMPENI ZA CCM USHETU

 

Naibu Katibu Mkuu wa CCM ( Bara) Ndugu Christina Mndeme akimnadi mgombea wa ubunge jimbo la Ushetu kwa tiketi ya CCM  Ndugu Emmanuel Cherehani (kulia) kwenye viwanja vya Nyamilangano. Chama Cha Mapinduzi kimezindua rasmi kampeni zake katika jimbo la Ushetu tarehe 26 Septemba 2021. (Picha na Adam Mzee/ CCM Makao Makuu).

Sehemu ya Watu waliojitokeza katika uzinduzi wa kampeni za CCM katika jimbo la Ushetu kwenye viwanja vya Nyamilangano. (Picha na CCM Makao Makuu).

NAIBU Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi  (Bara) Ndugu Christina Mndeme, leo amezindua kampeni za ubunge jimbo la Ushetu wilayani Kahama mkoa wa Shinyanga.

Mndeme, amesema mgombea huyo Emanuel Peter Cherehani, anatosha kurithi viatu vya aliyekuwa mbunge wa jimbo hilo ambaye pia alikuwa Waziri wa Ulinzi, marehemu Elias Kwandikwa.

Uzinduzi wa kampeni hizo umefanyika katika viwanja vya Nyamilangano, ambapo CCM kimetumia fursa hiyo kumsimamisha Ndugu Emmanuel Peter Cherehani na kumkabidhi Ilani ya Uchaguzi ya 2020/2025 ya Chama hicho.

Katika hatua hiyo, Mndeme alisisitiza kuwa Chererehani ana uzoefu wa uongozi katika kutetea maslahi ya wananchi wa Ushetu, hususani katika masuala ya kilimo, elimu, afya na maboresho ya miundombinu.

Aliongeza kuwa, mgombea huyo amekuwa Mwenyekiti wa vyama mbalimbali vya ushirika ikiwemo cha wakulima wa Tumbaku,Chama cha Mwadui na Ubangwa na mtetezi wa maendeleo ya wakulima wa pamba.

Katika mkutano huo viongozi mbalimbali wa Chama na Serikali walihudhuria akiwemo Katibu wa Oganaizesheni  wa CCM Ndugu Maudline Castiko, wabunge wa mkoa wa Shinyanga na mamia ya wananchi.


Naibu Katibu Mkuu wa CCM ( Bara) Ndugu Christina Mndeme  akiwaongoza wanachama wa CCM na wananchi kucheza muziki wa Chama kutoka bendi ya TOT kwenye viwanja vya Nyamilangano. Chama Cha Mapinduzi kimezindua rasmi kampeni zake katika jimbo la Ushetu terehe 26 Septemba 2021. (Picha na Adam Mzee)

Naibu Katibu Mkuu wa CCM ( Bara) Ndugu Christina Mndeme akimkabidhi Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2020/2025 mgombea wa ubunge jimbo la Ushetu kwa tiketi ya CCM  Ndugu Emmanuel herehani (kulia) kwenye viwanja vya Nyamilangano. Chama Cha Mapinduzi kimezindua rasmi kampeni zake katika jimbo la Ushetu terehe 26 Septemba 2021. (Picha na Adam Mzee)

No comments:

Post a Comment