WATU WENYE ULEMAVU WATAKIWA KUCHANGAMKIA MKOPO USIO NA RIBA - THE HABARII

ASAS GROUP

Habari Mpya


Tuesday 7 May 2019

WATU WENYE ULEMAVU WATAKIWA KUCHANGAMKIA MKOPO USIO NA RIBA

 Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge, Ajira, Vijana na Wenyeulemavu, Stellah Ikupa (kulia), akiwa meza kuu pamoja na Rais wa Umoja wa Wanamuzi Tanzania (TAMUFO), Dk. Donald Kisanga (katikati) na Mbunge wa Viti Maalumu, Amina Mollel kwenye Tamasha la Kitaifa la kupinga Unyanyasaji na Ukatili wa Kijinsia kwa Watuwenye Ulemavu lililoandaliwa na umoja  huo lililofanyika Jijijini Dodoma wiki iliyopita. 


Viongozi hao wakiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya washiriki wa Tamasha hilo.


Mtoto Bilal Donald Nyawenga mwenye ulemavu anayedaiwa kufungiwa tangu 1997.

Rais wa Umoja wa Wanamuzi Tanzania (TAMUFO), Dk. Donald Kisanga, akijaribu kuzungumza na mtoto huyo.

Na Mwandishi Wetu, Dodoma

WATU Wenyeulemavu wametakiwa kuchangamkia fedha za mkopo bila riba walizotengewa na Serikali ambazo zipo katika Halmshauri ya miji nchini.

Wito huo umetolewa na Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu,Sera, Bunge, Ajira, Vijana na Wenyeulemavu, Stellah Ikupa wakati akihutubia kwenye Tamsha la Kitaifa la kupinga Unyanyasaji na Ukatili wa kijinsia kwa watu wenye ulemavu lililoandaliwa na Umoja wa Wanamuzi Tanzania (TAMUFO) lililofanyika Jijijini Dodoma wiki iliyopita. 

"Changamukieni fedha hizo ambazo ni asilimia mbili zipo kwenye halmshauri zetu tena mnakopa bila ya kuwa riba yoyote waambieni na wenzenu" alisema Ikupa.

Alisema awali wanawake na vijana kila kundi lilitengewa asilimia 5 ya fedha kwa ajili ya kukopeshwa lakini baada ya waziri huyo na wenzake kuomba kusaidiwa walemavu kila kundi lilitoa asilimia moja na kuwa mbili kwa ajili ya watu wenye ulemavu.

Ikupa alisema Serikali imekuwa ikiwajali sana watu wenyeulemavu ndio maana imetenga wizara hiyo ambayo inashughulikia masuala yote yanayo wahusu walemavu.

Rais wa TAMUFO, Dkt. Donald Kisanga aliiomba serikali kuendelea kusimamia sheria zote zinazowalinda walemavu ikiwa pamoja na kuwajengea miundombinu mizuri kama ngazi za kushukia na kupandia katika majengo makubwa.

"Kumekuwa na ukihukaji wa sheria za kuwalinda walemavu kama kuwaficha majumbani na kukosa haki zao za msingi kama kupata elimu na huduma zingine za kijamii tunaiomba serikali iendelee kusimamia sheria hizo na kuchukua hatua kali kwa watuhumiwa" alisema Dk.Kisanga.

Baada ya Tamasha hilo wananchi waliweza kuwaongoza viongozi wa TAMUFO kwenda kumshuhudia mtoto Bilal Donald Nyawenga mwenye ulemavu ambaye yupo Kijiji cha Chogola Kata ya Sama wilayani Mpwapwa ambaye inadaiwa anafungiwa ndani  tangu azaliwe mwaka 1997.

Mtoto huyo mwenye ulemavu wa baadhi ya viungo vyake na mwenye kichwa kikubwa amekosa haki ya kusoma lakini licha ya baadhi ya viongozi wa kijiji hicho kujua changamoto aliyonayo hakuna hatua yoyote iliyochukulia ya kuweza kumsaidia.

No comments:

Post a Comment