SERIKALI YA MAREKANI YAZINDUA MRADI KUHIFADHI MAZINGIRA UKANDA WA MAGHARIBI TANZANIA - THE HABARII

ASAS GROUP

Habari Mpya


Monday 5 November 2018

SERIKALI YA MAREKANI YAZINDUA MRADI KUHIFADHI MAZINGIRA UKANDA WA MAGHARIBI TANZANIA

Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Jane Goodall (JGI – USA) Dk. Carlos Drews (kushoto) akipeana mkono na Waziri wa Nchi katika Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) January Makamba na Kaimu Balozi wa Marekani nchini Dk. Inmi Patterson (kati) baada ya uzinduzi wa mradi utakaogharimu kiasi cha dola za kimarekani milioni 20 ili kuboresha usimamizi katika kuhifadhi mazingira kwenye ukanda wa magharibi mwa Tanzania. Mradi huu mpya utasaidia watu wa Mikoa ya Kigoma na Katavi. (Picha: Ubalozi wa Marekani).


 
KAIMU Balozi wa Marekani nchini Tanzania Dkt. Inmi Patterson na  Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais wa Muungano na Mazingira Ndugu January Makamba wamezindua mradi utakaogharimu kiasi cha dola za kimarekani milioni 20 ili kuboresha usimamizi katika kuhifadhi mazingira kwenye ukanda wa magharibi mwa Tanzania. Mradi huu  wa uhifadhi wa mazingira unafadhiliwa na Serikali ya Marekani kupitia Shirika lake la Maendeleo ya Kimataifa (USAID) na utatekelezwa kwa ushirikiano wa pamoja na Taasisi ya Jane Goodall (JGI).

Mradi huu mpya utasaidia watu wa Mikoa ya Kigoma na Katavi, pamoja na serikali za mitaa, katika utekelezaji wa mipango ya matumizi bora ya ardhi na utakaonufaisha vijiji 104.

Mradi huu wa Uhifadhi wa Mazingira umeundwa kulinda mazingira wakati pia unasaidia wananchi katika shuhuli za kujikimu kiuchumi na maisha bora kama vile uzalishaji wa kahawa na utalii asili kwa ajili ya watanzania. Taasisi ya Jane Goodall itafanya kazi kwa karibu na jamii ili kuhamasisha mazoea endelevu zaidi ya usimamizi wa ardhi na kukuza elimu ya mazingira, kwa kutumia majukwaa kama vile mradi iliyofanikiwa sana ya Roots na Shoots ya Taasisi ya Jane Goodall.

Zaidi ya hayo, kama sehemu ya ruzuku hii, Taasisi ya Jane Goodall itaendelea kufanya kazi kwa kushirikiana na Serikali ya Tanzania katika kuunda mifumo imara zaidi katika kuhifadhi na kulinda sokwe walioko  ndani na nje ya maeneo tengefu.

No comments:

Post a Comment