Na Munir Shemweta, WANMM ARUSHA
MAWAKALA wa Milki nchini wametakiwa kujisajili katika mfumo wa Wizara ya Ardhi ili kuingia kwenye mfumo rasmi utakaowezesha kutambulika. Hayo yameelezwa Februari 12, 2025 na Mratibu wa Mjadala kuhusu Utambuzi na Usajili wa Wadau wa Sekta ya Milki Bi. Nuru Kimbe, mjadala uliofanyika mkoani Arusha.
Amesema, ni vizuri mawakala wa milki wakajisajili katika mfumo ili waweze kutambulika katika kipindi hiki ambacho wizara inategemea kuwa na sheria ya milki.
"Nasisitiza mawakala waweze kujisajili na waweke ‘details’ za masingi kama anuani na mahali wanapofanyia kazi". Amesema Bi. Nuru
Kwa mujibu wa Bi. Kimbe ambaye ni Afisa kutoka Kitengo cha Milki Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi, faida za kujisajili ni pamoja na kutambulika na serikali kitu alichokieleza kitarahisisha kazi kwa mawakala ambapo amesema hatua hiyo itarahisisha katika kazi zao kama wakala na kuwafikia wateja sambamba na kuaminika zaidi.
Amebainisha kuwa, kwa sasa mijadala inafanyika kwenye majiji ambako soko la milki linafanyika sana na kuitaja majiji hayo kuwa ni Dar es Salaam, Dodoma, Arusha na Mwanza.
Hata hivyo, amesema wako katika mchakato wa kufika mikoa mingine inayokuwa sana katika soko la milki kama vile Tanga, Morogoro, Pwani na Mbeya huku nia ikiwa ni kufika nchi nzima.
Kwa upande wake mmoja wa washiriki wa kikao hicho kutoka kampuni ya GimcoAfrika Ltd Bw. Herien Muro amesema, elimu waliyopata kupitia kikao kazj ni muhimu kwa kuwa inaenda kuondoa udanganyifu huku ikiisaidia serikali kupata mapato.
Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi kupitia kitengo cha Milki (REAL ESTATE) inaendesha mijadala ya pamoja na wadau kwa lengo la kupata maoni kuhusu utambuzi na usajili wa wadau wa sekta ya milki ili kuboresha na kukuza sekta ya milki nchini.
No comments:
Post a Comment