BALOZI IDDI: MUUNGANO UNA FURSA KWA WATANZANIA - THE HABARII

ASAS GROUP

Habari Mpya


Friday, 12 December 2025

BALOZI IDDI: MUUNGANO UNA FURSA KWA WATANZANIA

Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais Mhe. Mhandisi Hamad Yussuf Masauni akizungumza na Makamu wa Pili Mstaafu wa awamu ya saba ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar Mhe. Balozi Seif Ali Iddi alipomtembelea nyumbani kwake Zanzibar, Disemba 11,2025.

Makamu wa Pili Mstaafu wa awamu ya saba ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar Mhe. Balozi Seif Ali Iddi (wa kwanza kulia) akizungumza na Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais Mhe. Mhandisi Hamad Yussuf Masauni alipomtembelea nyumbani kwake Zanzibar, Disemba 11,2025 akiwa ameambatana na viongozi mbalimbali wa Ofisi ya Makamu wa Rais.

Mwandishi Wetu, Zanzibar

MAKAMU wa Pili wa Rais Mstaafu wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, Mhe. Balozi Seif Ali Iddi amesema uwepo wa Muungano umepanua wigo na fursa kwa wananchi katika nyanja za uongozi, biashara na ajira.

Mhe. Balozi Iddi ameyasema hayo wakati wa mazungumzo baina yake na Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Mhe. Mhandisi Hamad Yussuf Massauni alipomtembelea nyumbani kwake Zanzibar, Disemba 11, 2025 akielezea uzoefu, historia na fursa mbalimbali zilizopo kupitia Muungano.

Amesema utekelezaji wa masuala mbalimbali ya Muungano yanayoendelea kufanyika yametokana na utaratibu uliowekwa, na kuhimiza kila mwananchi kuwa msimamizi na kuwaasa baadhi ya watu wachache wasiolitakia mema Muungano.

“Kupitia vikao vya pamoja kati ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania (SJMT) na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar (SMZ), hilo limekuwa ni alama ya kila mmoja kuona namna bora ya kusimamia maslahi ya Muungano na sio upande mmoja.” Amesema Mhe. Balozi Iddi.

Kwa mujibu wa Balozi Iddi, ameeleza kuwa Muungano umechukuwa nafasi kubwa katika kuwaunganisha wananchi na kuimarisha mahusiano mazuri baina ya Tanzania Bara na Zanzibar na hivyo kuwawezesha wananchi mpana kwa wananchi kutumia fursa mbalimbali za kiuchumi, kisiasa na kijamii ili kujipatia maendeleo.

Aidha amesema kuwa Muungano umekuwepo kutokana na sababu mbalimbali ikiwemo mahusiano ya karibu na ya kihistoria katika nyanja mbalimbali kama vile udugu wa damu, biashara, utamaduni, lugha na mahusiano ya karibu kisiasa baina ya vyama vya TANU na ASP. 


No comments:

Post a Comment