DKT. MPANGO AWEKA JIWE LA MSINGI BARABARA YA KAZILAMBWA-CHAGU (KM 36) - THE HABARII

ASAS GROUP

Habari Mpya


Friday 11 October 2024

DKT. MPANGO AWEKA JIWE LA MSINGI BARABARA YA KAZILAMBWA-CHAGU (KM 36)

Makamu wa Rais, Dkt. Philip Mpango akivuta kitambaa kuashiria uwekaji wa jiwe la msingi la barabara ya Kazilambwa – Chagu (Km36) kwa kiwango cha lami, Oktoba 11, 2024 mkoani Tabora.

Makamu wa Rais, Dkt. Philip Mpango akimpongeza Naibu Waziri wa Ujenzi, Mhandisi Godfrey Kasekenya mara baada ya kuweka jiwe la msingi barabara ya Kazilambwa – Chagu (Km36) kwa kiwango cha lami, Oktoba 11, 2024 mkoani Tabora.

Muonekano wa sehemu ya barabara ya ya Kazilambwa – Chagu (Km36) kwa kiwango cha lami ambayo imewekwa jiwe la msingi na Makamu wa Rais, Dkt. Philip Mpango, Oktoba 11, 2024 mkoani Tabora.

Muonekano wa sehemu ya barabara ya ya Kazilambwa – Chagu (Km36) kwa kiwango cha lami ambayo imewekwa jiwe la msingi na Makamu wa Rais, Dkt. Philip Mpango, Oktoba 11, 2024 mkoani Tabora.

MAKAMU wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Philip Mpango ameweka jiwe la msingi Barabara ya Kazilambwa- Chagu na kusisitiza umuhimu wa wananchi kuzilinda Barabara  na alama za Barabarani ili kuepuka ajali.


Akizungumza na wananchi wa  Ugansa wilayani Kaliua, mkoani Tabora,  Oktoba 11, 2024, Dkt. Mpango amehimiza pia umuhimu wa walimu kuwafundisha wanafunzi matumizi sahihi ya barabara.


" Serikali inatumia fedha nyingi kujenga barabara pamoja na kuweka alama za barabarani, hivyo wajibu wenu ni kuzitunza na kuzilinda ili zisiharibike kwa haraka“, amesisitiza Dkt. Mpango.


Dkt. Mpango amewataka wataalam wote wanaosimamia ujenzi huo kuhakikisha wanasimamia thamani ya fedha na kukamilika kwa wakati.


Aidha, kuhusu usalama barabarani Dkt. Mpango ametoa rai kwa madereva na watumiaji wa vyombo vya moto nchini kuzingatia alama za barabarani ili kuepusha ajali na kuwaonya wale wanaohujumu alama za barabarani kuwa hatua za kisheria zitachukuliwa dhidi yao.


Kwa upande wake Naibu Waziri wa Ujenzi Eng. Godfrey Kasekenya amesema ujenzi wa barabara ya Kazilambwa-Chagu (Km 36) na Ugansa-Usinge (Km 7.41) ni muendelezo wa juhudi za Serikali kuifungua nchi katika kuboresha huduma za usafiri na uchukuzi na hivyo kuleta tija kwa wananchi.


" Mheshimiwa Makamu wa Rais  tumejipanga kuhakikisha mkoa wa Tabora na Kigoma inaunganishwa kwa lami katika kipindi kifupi kijacho na hivyo kuweka historia mpya kwa wananchi wa  mikoa hiyo",  amefafanua  Mhandisi, Kasekenya.


Naye, Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Barabara nchini (TANROADS), Eng. Mohamed Besta amesema ujenzi wa barabara ya Kazilambwa-Chagu (Km 36) ni sehemu ya barabara ya Kaliua-Malagarasi-Ilunde Km 156 ambapo kukamilika kwake kutaunganisha mkoa wa Tabora na Kigoma kwa lami na wamejipanga kuhakikisha ujenzi unakamilika kwa wakati na ubora uliokusudiwa.


Makamu wa Rais amemaliza ziara yake ya siku 3 mkoani Tabora kwa kukagua na kuweka mawe ya msingi katika miradi mbalimbali ikiwemo barabara, kiwanja cha ndege, maji, umeme na majengo.


No comments:

Post a Comment