Serikali imesaini Mkataba wa ujenzi wa barabara ya Kahama-Bulyanhulu Jct - Kakola (km 73) kwa kiwango cha lami ili kufungua fursa za kiuchumi za madini, Kilimo, Misitu na Utalii katika mikoa ya Shinyanga, Geita, Tabora, Kagera na Kigoma.
Mkataba huo umesainiwa
kati ya Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) na kampuni ya China Civil
Engineering Construction Corporation kwa gharama ya Shilingi Bilioni 101.2 kwa
ufadhili wa Kampuni ya Madini ya Barrick Tanzania Mining Companies (BTMCs) na
Serikali ya Tanzania.
Akishuhudia Utiaji
Saini wa barabara hiyo Wilayani Kahama Mkoani Shinyanga, Waziri wa Ujenzi,
Innocent Bashungwa ameeleza kuwa barabara hii imekuwa ni kilio cha muda mrefu
na sasa Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa ushirikiano mzuri na wawekezaji
wa ndani ya nchi ikiwemo kampuni ya Barick ametoa kibali barabara hiyo iweze
kuanza kujengwa kwa kiwango cha lami.
“Niwashukuru Barrick
kwa ushirikiano ambao mmetupa kwa ujenzi wa hizi kilometa 73 na kwa hilo
niwahakikishie wananchi tumewaletea Mkandarasi ambaye ni mbobezi na mwenye
uwezo mkubwa na kwa namna tulivyojipanga na usimamizi makini nitakaouweka
kwenye hii barabara msiwe na wasiwasi tutatimiza utekelezaji wake ndani ya miezi
27 na si zaidi ya hapo”, amesema Bashungwa
Aidha, Bashungwa
ameeleza kuwa Mhe. Rais pia ameelekeza Wizara ya Ujenzi kuanza hatua za kuanza
kujengwa kwa kiwango cha lami barabara ya kutoka Iloginhadi Mtakuja (km 57.4) ambayo
ni barabara ya kiuchumi na inaunganisha Mkoa wa Shinyanga na Geita.
Bashungwa amemuagiza
Mtendaji Mkuu wa TANROADS kwa
kushirikiana na Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Barabara za Mijini na Mijini
(TARURA) kuona namna ya kuboresha miundombinu ya barabara za Mji wa Kahama ili
kuusaidia mji huo katika ukuaji wake wa Kiuchumi na kijamii.
Aidha, Bashungwa
amewahakikishia wananchi kuwa mtandao wa barabara kwa zile za changarawe na
zile za lami zilizopo Mkoani Shinyanga zitaendelea kusimamiwa na kuhudumiwa ili ziweze kupitika
msimu wa kiangazi na vuli ikiwemo barabara ya Old Shinyanga - Solwa - Burige
mpaka Kahama pamoja na ile Kolandoto-Lalago.
Bashungwa amemtaka
Mkandarasi huyo kuona namna ya kuchangia huduma za kijamii kwa wananchi
wanaouzunguka mradi huo pamoja na kushirikiana na wananchi wakati wa
utekelezaji wa mradi.
No comments:
Post a Comment