DAWATI LA KUSHUGHULIKIA UKATILI WA KIJINSIA LAZINDULIWA TIA MKOA SINGIDA - THE HABARII

ASAS GROUP

Habari Mpya


Thursday 2 November 2023

DAWATI LA KUSHUGHULIKIA UKATILI WA KIJINSIA LAZINDULIWA TIA MKOA SINGIDA

Mkuu wa Dawati la Jinsia wa Jeshi la Polisi Mkoa wa Singida, Mkaguzi wa Polisi Amina Abdallah, ambaye alikuwa mgeni rasmi akizungumza na Wanafunzi wa Taasisi ya Uhasibu Tanzania (TIA) Kampasi ya Singida wakati akizindua rasmi dawati la jinsia Oktoba 1, 2023.

Na Dotto Mwaibale, Singida

JESHI la Polisi Mkoa wa Singida limezindua rasmi dawati la jinsia katika Taasisi ya Uhasibu Tanzania (TIA) Kampasi ya Singida kwa lengo la kukabiliana na vitendo vya ukatili wa kijinsia kwa wanafunzi wa taasisi hiyo.

Mkuu wa Dawati la Jinsia wa Jeshi la Polisi mkoani hapa, Mkaguzi wa Polisi Amina Abdallah ambaye alikuwa mgeni rasmi na kuongozana na Koplo Eva Julius wa dawati hilo, akizungumza Novemba 1, 2023 kwenye uzinduzi huo alisema dawati hilo litasaidia kwa wanafunzi wanaopatwa na madhira kutoa taarifa ili changamoto zao ziweze kufanyiwa kazi.

Alisema viongozi wa dawati hilo ambao watakuwa wanapokea taarifa kabla ya kuzifikisha ngazi za juu wazingatie suala la usiri ili wanafunzi waweze kuwa na imani na dawati hilo.

Abdallah alipongeza uongozi wa taasisi hiyo kwa kazi nzuri ambayo imesaidia kudhibiti vitendo vya unyanyasa wa kijinsia katika msimu wa masomo uliopita hakujaripotiwa  matukio ya unyanyasaji wa kijinsia yakiwamo ya ubakaji na ulawiti ikilinganishwa na kipindi cha nyuma.

" Huu utaratibu wa kuwa na dawati la kijinsia usiishie katika taasisi hii bali uenezwe katika vyuo vingine na shule za msingi kwa kutoa elimu ya kupinga vitendo vya ukatili wa kijinsia na hiyo ndio itakuwa njia nzuri ya kukabiliana na matukio hayo," alisema Abdallah.

Katika kuhakikisha dawati hilo linapata nguvu kushughulikia changamoto za unyanyasaji wa kijnsia kwa  wanafunzi walichaguliwa wajumbe watatu kusimamia ambao ni Waziri wa Afya kutoka Serikali ya Wanafunzi ya taasisi hiyo, Ramla Mchomvu, Mkutubi Francis Majele na Mlezi wa wanafunzi, Asia Hansy, 

Makamu Mkuu wa Taasisi hiyo, Flora Lemnge aliwataka wanafunzi hao watakapokuwa na changamoto yoyote ya ukatili wa kijinsia kwenda kutoa taarifa kwa wajumbe hao ambao ni wasiri na wanauzoefu mkubwa ambapo kwa wavulana aliwataka kwenda kumuona Mkutubi Francis Majele. 

Mshauri wa wanafunzi katika taasisi hiyo, Ambwene Kajula alisema wanafuraha kulizindua dawati hilo licha ya kuwa nalo na kuwa lengo la kulizindua ni kutaka kuukataa na kuutokomeza kabisa ukatili katika jamii yao na watu wawe bora kama Rais Dk. Samia Suluhu Hassan alivyoamua kuweka Wizara ya Ustawi wa Jamii na kuona kazi ya dawati la jinsia lina msaada mkubwa.

"Dawati la jinsia linasaidia kuweka mazingira bora kwa wanafunzi na kama wataweza kuongea na kupata sehemu ya kusema madhira yao walioyapata kwa ukaribu tena kwa mtu ambaye amemzoea ni jambo jema sana," alisema Kajula.

Alisema katika kampasi hiyo wamechaguliwa baadhi ya walimu na watumishi kuwa wajumbe wa dawati hilo ambao watasaidia kupokea taarifa kutoka kwa waathirika na kuzifanyia kazi na kuyafikia malengo ya kutokomeza ukatili katika taasisi hiyo na nchi kwa ujumla.

Mwanafunzi wa taasisi hiyo anayesomea ngazi ya cheti, Pendo Maube akizungumza kwa niaba ya wenzake alisema kupitia uzinduzi huo wameweza kujua fursa mbalimbali ambazo zinapatikana katika dawati hilo la kijinsia kama kujua haki zao na namna ya utoaji wa taarifa pale panapotokea changamoto ya ukatili wa kijinsia.

Katika uzinduzi huo elimu mbalimbali zilitolewa ambapo Mkaguzi wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji Mkoa wa Singida, Mwantumu Bakari akiongozana  na wataalamu wa jeshi hilo walitoa mafunzo ya kukabiliana na majanga ya moto ambapo walitoa namba ya kutoa taarifa iwapo kutatokea changamoto hiyo kwa kupiga namba 114.

Aidha, viongozi mbalimbali wa Shujaa wa Maendeleo na Ustawi wa Jamii (SMAUJATA) mkoani hapa nao walipata fursa ya kutoa elimu ya kupinga vitendo vyote vya ukatili na walitoa namba 116 ya kupiga kwa ajili ya kutoa taarifa za vitendo vya ukatili ambapo wanafunzi hao walikubali kuwa mashujaa wa Smaujata.

No comments:

Post a Comment