![]() |
| Waziri wa Ujenzi Innocent Bashungwa kulia akiwa katika ziara yake kukagua miundombinu ya barabara Wilaya ya Kigamboni. |
![]() |
| Waziri wa Ujenzi Innocent Bashungwa kulia akiwa katika ziara yake kukagua miundombinu ya barabara Wilaya ya Kigamboni. |
![]() |
| Ziara ikiendelea. |
SERIKALI ipo katika hatua za mwisho za maandalizi
ya ujenzi kwa kiwango cha lami wa Barabara ya Kibada-Mwasonga-Kimbiji yenye
urefu wa Km 41 wilayani Kigamboni.
Waziri wa Ujenzi Innocent Bashungwa amesema hatua
hiyo ni mwendelezo wa juhudi za Serikali za kuiwezesha Wilaya ya Kigamboni kuwa
na barabara nyingi za lami na hivyo kuchochea maendeleo ya kijamii na kiuchumi
kwa wakazi wake.
"Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan amenituma
nije nikague barabara hii ambayo ujenzi wake utaanza hivi karibuni", amesema
Bashungwa.
Aidha, amemuagiza Meneja wa Wakala wa Barabara
(TANROADS) Mkoa wa Dar es Salaam, Eng. John Mkumbo kuendelea kuikarabati
barabara hiyo ili ipitike wakati wote wakati maandalizi ya kuijenga kwa lami
yakiendelea.
Kufuatia ombi la Mkuu wa Wilaya ya Kigamboni, Halima
Bulembo la kuiomba Serikali kujenga kipande cha Km 7, kutoka Kimbiji hadi Cheka
ambacho ni muendelezo wa barabara hiyo, Waziri Bashungwa amamuagiza Meneja wa
TANROADS Mkoa wa Dar es Salaam kufanya usanifu katika sehemu hiyo wakati yeye
akifuatilia kibali cha Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ili kuiwezesha barabara
yote kujengwa kwa lami.
Kaimu Mtendaji Mkuu wa TANROADS, Eng. Dorothy
Mtenga amesema Barabara hiyo ni moja ya barabara za muhimu kwa Mkoa wa Dar-es
Salaam kwani inapita sehemu zenye uwekezaji
na idadi kubwa ya watu.
"Barabara hii ikikamilika itachochea uchumi wa
wananchi wa Kigamboni na kutengeneza mtandao mzuri wa barabara za lami ",
amesisitiza Eng. Mtenga.
Waziri Bashungwa amehitimisha ziara yake ya siku
tatu jijini Dar-es Salaam ambapo pamoja na mambo mengine ametembelea Wilaya
zote 5 za mkoa huo ambazo ni Ilala, Kinondoni, Temeke, Ubungo na Kigamboni na
kukagua athari za mvua za vuli na kutoa maelekezo kwa TANROADS, Wakandarasi na wananchi hususan kutovamia
maeneo ya hifadhi ya barabara na kuzilinda barabara ili zidumu kwa muda mrefu.
IMETOLEWA NA KITENGO CHA HABARI NA MAWASILIANO
WIZARA YA UJENZI






No comments:
Post a Comment