KAMATI YA BUNGE YA MIUNDOMBINU YAPONGEZA UTENDAJI WA UCSAF - THE HABARII

ASAS GROUP

Habari Mpya


Saturday 13 February 2021

KAMATI YA BUNGE YA MIUNDOMBINU YAPONGEZA UTENDAJI WA UCSAF

Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Dkt. Faustine Ndugulile akiwasilisha majukumu ya Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote kwa wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu, Bungeni, Dodoma. Wa kwanza kulia ni Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Selemani Kakoso na wa kwanza kushoto ni Naibu Waziri wa Wizara hiyo, Mhandisi Kundo Mathew.





Na Prisca Ulomi, WMTH

KAMATI ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu yapongeza utendaji mzuri wa Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote (UCSAF) baada ya Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Dkt. Faustine Ndugulile kuwasilisha taarifa ya majukumu ya Mfuko huo kwa wajumbe wa Kamati hiyo wakati wa kikao cha Waziri huyo na Kamati hiyo kilichofanyika Bungeni Dodoma.


Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu, Selemani Kakoso ametoa pongezi hizo kwa viongozi wa Wizara, Menejimenti ya Wizara na watendaji wa UCSAF kwa kazi nzuri inayofanyika ya kutoa huduma ya mawasiliano kwenye taifa letu ikiwa ni pamoja na kupeleka vifaa vya TEHAMA mashuleni na kufundisha waalimu namna ya kutumia vifaa hivyo kufundushia na wanafunzi kujifunzia. 


Amesema kuwa lengo la kikao hicho ni kufanya semina ya kuwajengea uwezo na uelewa wajumbe wa Kamati hiyo ili wafahamu majukumu ya UCSAF ili waweze kushirikiana na Wizara kuhakikisha kuwa UCSAF inatekeleza majukumu yake na kufikia malengo iliyojiwekea.


Ameongeza kuwa wabunge wataishauri Serikali kuongeza mapato ya UCSAF ili kuhakikisha kuwa UCSAF inakuwa na bajeti nzuri ya kuendelea kufikisha huduma za mawasiliano maeneo mbali mbali nchini hususan maeneo ya pembezoni na mipakani kwa kuwa nchi yetu ni kubwa.


Dkt. Faustine Ndugulile amesema kuwa Wizara yake inasimamia njia moja kuu za uchumi kama ilivyo Wizara ya Ujenzi inavyobeba barabara na Nishati inabeba umeme, na hii ni moja ya njia kuu za uchumi katika dunia ambayo tunakwenda nayo ili tuhakikishe kuwa tunajenga uchumi wa kidijitali kwa kuwa sasa hivi dunia imehamia kiganjani na Wizara hii itaratibu masuala yote ya TEHAMA ndani ya Serikali ili mwananchi apate huduma kwa wakati na TEHAMA ichangie kikamilifu pato la taifa.


Naibu Waziri wa Wizara hiyo, Mhandisi Kundo Mathew amefafanua kuwa Wizara kwa kushirikiana na UCSAF na kampuni za simu za mkononi wataendelea kuboresha huduma za mawasiliano kwenye maeneo mbali mbali nchini kwa kuongeza uwezo wa minara ya mawasiliano ili iweze kutoa huduma nzuri ya sauti na data kutoka teknolojia ya 2G na kuwa teknolojia ya 3G au 4G. 


Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa, Humphrey Polepole ambaye ameshiriki kikao hicho, ameipongeza UCSAF kwa kujenga vituo vya TEHAMA kwenye kisiwa cha Unguja na Pemba ambapo vituo hivyo vinawawezesha wananchi kupata huduma ya intaneti karibu na maeneo yao na ameshauri ujenzi wa vituo hivyo uendelee kufanyika katika maeneo mbali mbali nchini.


Mtendaji Mkuu wa UCSAF, Justina Mshiba amesema kuwa UCSAF itapita kwenye maeneo yote ya mipakani mwa Tanzania na kufanya tathmini ili kupata idadi ya minara inayohitajika kwenye maeneo hayo ili kuhakikisha kuwa maneo ya mipakani yana mawasiliano ya uhakika na usalama wa kutosha kwa kuwa mawasiliano yanabeba usalama wa taifa letu.


No comments:

Post a Comment