NA LUSUNGU HELELA-KILIMANJARO
NAIBU Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe.Constantine Kanyasu amewashauri wabeba mizigo na waongoza watalii katika Mlima Kilimanjaro wapunguze utitiri wa vyama walivyoviunda vya kutetea maslahi yao badala yake wabaki na vyama viwili ambavyo vitakuwa na nguvu ya kudai haki na kupigania maslahi yao.
Pia ameyataka Makampuni ya watalii kuwalipa malipo yao wabeba mizigo na waongoza watalii kwa mujibu wa sheria badala ya kuwapunja malipo yao huku wakidai kuwa malipo hayo hayatekelezeki kisheria. Kwa mujibu wa sheria waongoza watalii katika mlima huo wanapaswa kulipwa si chini ya Dola 20 za Marekani kwa siku sawa na mbeba mizigo Dola 10 za Marekani kwa siku.
Aidha, Amewataka wabeba mizigo na waongoza watalii hao wawe wanatoa taarifa kwa siri kwa yale makampuni yanayowalipa pesa kidogo na kwamba yale Makampuni yatakayobainika yafutwe kwa kosa la kukiuka sheria hiyo.
Hayo yamebainishwa na Naibu Waziri huyo wakati alipokuwa akizungumza na wadau wa Utalii katika Mkoa wa Kilimanjaro wakati alipofanya ziara kutembelea Hifadhi ya Taifa ya Mlima Kilimanjaro lengo likiwa ni kutafutia ufumbuzi kero mbalimbali zinazowakabili wadau hao katika sekta ya Utalii. Amesema haiwezekani vyama zaidi ya nane vikawa vinafanya kazi moja ya kupigania na kudai maslahi ya wabeba mizigo na waongoza watalii halafu kukawa na ufanisi kwanza.
Daniel Maro, mbeba mizigo ya watalii amemueleza Naibu Waziri huyo kuwa wamekuwa wanalipwa na baadhi ya Makampuni ya watalii malipo kiduchu ya kiasi cha shilingi 5,000 na muda mwingine shilingi 8,000 badala ya elfu 20,000 kwa siku. Amesema malipo hayo ni madogo sana ukilinganisha na ugumu wa kazi hiyo na wamekuwa hawana pa kulalamikia na wale wote ambao wamekuwa wakibainika kulalamika wamekuwa wakikosa kupata kazi tena kutoka kwenye kampuni hayo.
Naye, Walter Mbambwo ambaye ni Muongoza watalii katika Mlima huo amesema kutokana na tatizo la ajira wamekuwa wakilazimika kutoa rushwa ya kiasi shilingi 20,000 ili wapate kazi hiyo lakini wamekuwa wakilipwa kiasi cha shilingi 5,000 au 8,000 tu.
Katika hatua nyingine, Mhe.Kanyasu amekitaka Chuo cha Usimamizi wa Wanyamapori cha Mweka kiangalie uwezekano wa kusambaza mtaala wa Waongoza watalii kwa vyuo vingine ikiwemo Chuo cha Taifa cha Taifa cha Utalii pamoja na VETA ili kuweza kutoa fursa kwa wadau hao kuweza kusoma mahali popote nchini badala ya utaratibu uliopo sasa unaowalazimisha kuwa lazima wasome katika Chuo hicho pekee nchini huku akiwaahidi kuwa suala la ukubwa wa ada wanayotozwa atalifanyia kazi.
Awali, Mkuu wa Wilaya ya Moshi, Mhe. Kippi Warioba amewahakikishia wadau hao kuwa ofisi yake ipo wazi kwa ajili ya kuwasaidia ili kuifanya sekta ya utalii katika mkoa wake uendelee kufanya vizuri. Hata hivyo amewataka waongoza watalii na wabeba mizigo ya watalii kuachana na vyama vile vinavyolenga kuwakandamiza badala ya kupigania maslahi yao wakati ofisi yake ikiangalia namna ya kuwasaidia namna ya kuondokana na kulipwa ujira mdogo.
No comments:
Post a Comment