WANAFUNZI KOROGWE GIRLS WAISHUKURU SERIKALI, TEA KUWAPATIA MAFUNZO YA AMALI - THE HABARII

THE HABARII

HABARI | MATUKIO | MICHEZO.


ASAS GROUP

Habari Mpya


Tuesday, 18 August 2026

WANAFUNZI KOROGWE GIRLS WAISHUKURU SERIKALI, TEA KUWAPATIA MAFUNZO YA AMALI

Mwanafunzi wa Shule ya Sekondari ya Wasichana ya Korogwe mkoani Tanga, Ntuli Danken,  akizungumza na waandishi wa habari waliotembelea banda la TEA  kwenye  Maonesho ya Wiki ya Taifa ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu 2026, yanayofanyika katika Viwanja vya Usagara, Jijini Tanga Agosti 17, 2026.

Na Mwandishi Wetu, Tanga

WANAFUNZI wa Shule ya Sekondari ya Wasichana ya Korogwe mkoani Tanga, wameishukuru Wizara ya Elimu kupitia Mamlaka ya Elimu Tanzania (TEA) kwa kuwapatia vifaa vya mafunzo ya Amali.

Pongezi hizo wamezitoa wakati wakizungumza na waandishi wa habari waliotembelea banda la TEA  kwenye  Maonesho ya Wiki ya Taifa ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu 2026, yanayofanyika katika Viwanja vya Usagara, Jijini Tanga Agosti 17, 2026.

“ Tunaishukuru Serikali kwa kutupatia mafunzo ya Amali na vifaa vya kujifunzia kwa mfano mimi nasomea mapishi ya aina mbalimbali naamini nikirudi nyumbani nitafanya shughuli zangu kitaalamu,” alisema Ntuli Danken mwanafunzi wa kidato cha tatu katika shule hiyo.

Alisema mafunzo ya Amali yana fursa nyingi kwani mwanafunzi akimaliza masomo yake ya kidato cha nne anaweza kujiajiri au kuajiriwa na hata anapokuwa akisubiri matokeo yake ataweza kujiingizia kipato.

Ntuli alisema changamoto iliyopo kwa baadhi ya wazazi ni kuwakataza watoto wao wasisome Amali kwa madai kuwa haina faida yoyote jambo ambalo siyo la kweli.

“Mwanafunzi akifeli iwapo atakuwa amejifunza Amali itamsaidia kufanya shughuli zake na kupata fedha za kumsaidia katika maisha yake ya kila siku,” alisema Ntuli.

Mwanafunzi mwingine wa shule hiyo, Najma Baraka wa kidato cha tatu ambaye naye anasoma Amali aliishukuru Serikali na TEA kwa kuwapelekea vifaa vya kujifunzia masomo ya Amali.

  “Zamani kabla ya kuletewa vifaa tulikuwa tunajifunza bila ya vitendo lakini sasa tunaweza kutengeneza bidhaa mbalimbali kutokana na vifaa tulivyo letewa,” alisema Najma.

Alisema masomo ya Amali yanawasaidia sana na atakapo maliza masomo yake ya kidato cha nne atakuwa na vyeti viwili cha NECTA na Amali ambapo kabla matokea hayajatoka atakuwa akitengeneza na kuuza bidhaa zake mbalimbali.

Mwalimu Catherine Machugu wa shule hiyo ambaye anafundisha masuala ya mapishi wanafunzi wa kidato cha tatu ameishukuru Serikali kupitia TEA kwa kuwafadhili vifaa mbalimbali ambavyo vinawasaidia wanafunzi walio mkondo wa Amali kusoma kwa ufanisi na uelewa zaidi.

Alisema shule hiyo ina jumla ya Amali 5 na ilipokea vifaa vyenye thamani ya zaidi ya milioni 400 kwa ajili ya Amali hizo ili kuboresha mazingira ya ujifunzaji na ufundishaji

“Vifaa hivi vimesaidia kuongezeka kwa usajili wa wanafunzi tofauti na hapo awali,” alisema Mwalimu Machugu.


Mwanafunzi wa Shule ya Sekondari ya Wasichana ya Korogwe mkoani Tanga, Najma Baraka,  akizungumza kwenye Maonesho hayo.

Mwalimu Catherine Machugu wa shule hiyo, akizungumzia msaada waliopatiwa na Serikali kupitia TEA.
Wanafunzi Najma Baraka (kushoto) na Ntuli Danken wakizungumza na waandishi wa habari (hawapo pichani waliotembelea banda la TEA.
Maafisa Miradi wa TEA Kabula Jullu na Joyce Minja (kulia), wakizungumza na wananchi waliotembelea banda la TEA kwenye Maonesho hayo.
 

No comments:

Post a Comment