TANZANIA YATHIBITISHA DHAMIRA YAKE KUIMARISHA UAMINIFU,
MIUNDO THABITI NA UTEKELEZAJI CHINI YA
GLOBAL AFRICA INVESTMENT SUMMIT
UZINDUZI rasmi wa Global Africa Investment Summit (GAIS), unaashiria mabadiliko ya
kimkakati jinsi Afrika inavyoshirikiana kupata mitaji ya kimataifa kwa kuzingatia
uwekezaji uliopangwa kwa viwango vya kitaasisi, unaoendana na vipaumbele vya kitaifa
na faida za muda mrefu.
Uzinduzi huo, uliofanyika ulifanyika jana, Jumanne usiku, kando ya World Governments
Summit jijini Dubai, uliwakutanisha baadhi ya Wakuu wa Nchi za Afrika, watunga sera,
wawekezaji wa kimataifa na viongozi wa biashara, kutambua kwamba changamoto ya
ukuaji wa Afrika si ukosefu wa rasilimali, bali ni miundo, na kwamba pengo hilo sasa
linashughulikiwa kwa kimkakati zaidi.
Katika hotuba yake, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania, alithibitisha utayari wa Tanzania kushiriki GAIS kama mshirika
wa kuaminika na wa muda mrefu katika uwekezaji.
“Kile wawekezaji wanachotafuta leo si fursa pekee, bali ni uaminifu - uaminifu kwa taasisi,
uthabiti wa sera, na serikali zinazotekeleza ahadi zake.”
Rais Samia alitolea mfano uwekezaji wa makusudi wa Tanzania katika miundombinu ya
msingi, yaani nishati, usafirishaji na uchukuzi - ili kuchochea uzalishaji, viwanda na
ujumuishaji wa kikanda.
2/3
Miradi mikubwa katika umeme wa maji, reli ya kisasa, bandari na barabara, sambamba
na Maeneo Maalum ya Kiuchumi (SEZs) na Kituo cha Huduma za Uwekezaji cha Dirisha
Moja, (TISEZA), imepunguza vikwazo kwa wawekezaji na kuimarisha imani yao kwa
Tanzania.
Aliongeza kuwa majukwaa kama GAIS yanaiwezesha Afrika, hususan Tanzania,
kuhama kutoka utamaduni wa kutangaza miradi isiyoungana na kuhamia katika
ushirikiano unaoendana na vipaumbele vya maendeleo ya Taifa, na matarajio ya
wawekezaji.
Zaidi ya Mkutano, GAIS imejipambanua kama mwezeshaji wa miundombinu ya soko,
mwenye lengo la kubadilisha mali za umma na za kitaifa za Afrika kuwa maeneo ya
uwekezaji yaliyoandaliwa vyema, yasiyo na madhara kubwa kibiashara, yanayokidhi
viwango vya kimataifa vya utawala, na usimamizi wa athari zinazoweza kuathiri faida.
Akizungumza katika uzinduzi huo, Dkt. Akinwumi Adesina, Mwanzilishi Mwenza na
Mwenyekiti Mtendaji wa GAIS pamoja na Rais wa zamani wa Benki ya Maendeleo ya
Afrika, alisema: “Tatizo si ukosefu wa rasilimali, bali ni ukosefu wa miundo ya
kuaminika inayounganisha rasilimali hizo na mitaji ya kimataifa.”
Alibainisha kuwa rasilimali za kimkakati za Afrika katika nishati, madini, miundombinu
na mtaji wa asili bado hazijathaminiwa ipasavyo kutokana na miundo dhaifu, taarifa
zisizo kamilifu, mifumo ya utawala iliyogawanyika na gharama kubwa za tathmini ya
uwekezaji (due diligence).
GAIS inalenga kushughulikia vikwazo hivyo kwa kuongeza uwezo wa kukuza miradi,
kutabirika na kuwa na ushirikiano wa muda mrefu.
“Afrika lazima ihame kutoka utegemezi wa misaada kwenda ukuaji unaoongozwa na
uwekezaji,” alisisitiza.
Mheshimiwa João Lourenço, Rais wa Angola na Mwenyekiti wa Umoja wa Afrika,
alisema GAIS inaakisi ukomavu wa kisiasa wa Afrika na utayari wake wa kushirikiana
na mitaji ya kimataifa kwa uwajibikaji na ushindani.
“Afrika lazima ichukue umiliki mkubwa wa mali zake za kitaifa na kuzitumia kwa njia
zinazoharakisha maendeleo,” alisema Rais Lourenço.
Aidha, alisisitiza umuhimu wa sheria zinazotabirika, mikataba yenye uwazi, na uthabiti
wa sera, akitaja mageuzi ya Angola, ikiwemo ubinafsishaji, dirisha moja la uwekezaji, na
miradi ya mpito wa nishati, kama ushahidi wa dhamira ya mageuzi na utekelezaji.
Wakati huohuo, Mheshimiwa John Mahama, Rais wa Jamhuri ya Ghana, alisisitiza haja
ya Afrika kubadili namna mitaji ya kimataifa inavyoshirikiana na bara hili, akisema:
“Afrika haina upungufu wa rasilimali. Kinachohitajika ni usanifu unaoruhusu mali hizo
kuzungumza lugha ya mitaji ya kimataifa.”
3/3
Alitaja mageuzi ya sekta ya dhahabu na madini nchini Ghana, ikiwemo kudhibiti
usafirishaji wa madini ghafi, kama mifano ya jinsi uundaji upya wa mali na uongezaji
thamani vinavyoweza kufungua mapato, ajira na viwanda, na kuongeza kuwa GAIS
itatoa usanifu unaoeleweka na mitaji ya kimataifa, sambamba na udhibiti wa vihatarishi
vya utekelezaji.
Kwa Tanzania, GAIS inatarajiwa kutoa fursa ya kimkakati ya kuvutia mitaji binafsi na ya
taasisi katika sekta za kipaumbele, kupunguza shinikizo kwa fedha za umma kupitia
ubia wa sekta ya umma na binafsi (PPP), ubia wa kibiashara (joint ventures), Vyombo
Maalum vya Utekelezaji (SPVs) na fedha mchanganyiko (blended finance), sambamba na
kuharakisha viwanda, kuongeza mauzo ya nje na kutengeneza ajira kwa vijana.
Hivyo, Tanzania itaweka mkazo katika maeneo matatu yanayohusiana:
1. Bandari, uchukuzi na biashara ya Kikanda kwa kutumia ukanda wake wa pwani
na mtandao wa bandari kama lango la Afrika Mashariki na Kati;
2. Nishati na Maeneo ya Viwanda, kwa kuimarisha uzalishaji, uongezaji thamani na
usalama wa nishati; na
3. Nafasi ya kuwa mhimili ndani ya Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC), kwa
kuiweka Tanzania kuwa kitovu cha kikanda cha uzalishaji, usafirishaji na
uchukuzi na uwepo wa nishati ya kutosha na ya Uhakika.
Kwa mtazamo wa kutoka utegemezi wa misaada kwenda katika ukuaji unaoongozwa na
uwekezaji, GAIS inafungua njia za ajira kwa vijana, uhamishaji wa ujuzi, ukuaji wa
biashara za ndani, pamoja na kukuza ushiriki wa mitaji binafsi.
TAARIFA KWA MHARIRI
Global Africa Investment Summit (GAIS) ni jukwaa la uwekezaji la bara la Afrika
lililoanzishwa kwa pamoja na Dkt. Akinwumi Adesina, Rais wa zamani wa Benki ya
Maendeleo ya Afrika, na Bi. Margery Kraus, Mwanzilishi na Mwenyekiti Mtendaji wa
APCO Worldwide.
Mkutano wa kwanza wa Global Africa Investment Summit unatarajiwa kufanyika
baadaye mwaka 2026.
Bakari S. Machumu
Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais, Ikulu.
.jpeg)


No comments:
Post a Comment