NAIBU Waziri wa Ujenzi Mteule, Mha. Godfrey Kasekenya amewataka watumishi wa Bodi ya Usajili Wa Wabunifu Majengo na Wakadiriaji Majenzi Nchini (AQRB) kufanya kazi kwa ushirikiano na kutatua changamoto zao katika maeneo yao ya kazi ili kuongeza weledi kwenye utendaji.
Ameyasema hayo alipokua akifungua kikao cha wafanyakazi wa Bodi hiyo, kilichofanyika katika Ukumbi wa Wakala wa Majengo Tanzania (TBA), Jijini Dodoma, ambapo ameeleza miongoni mwa manufaa ya ushirikiano na umoja kazini ni pamoja na kuifanya taasisi kutoa huduma za viwango kwa wadau.
“Vikao kama hivi vinasaidia watu kuondokana na mazingira ya utendaji ya kawaida sababu mnakaa pamoja mnafahamiana vizuri kitabia, mnajitathmini na kuja na suluhu ya utatuzi wa changamoto ambazo zinakabili taasisi maana vinahusisha kila kada zote, tumieni vizuri fursa hii ‘ amesema Kasekenya.
Akifafanua umuhimu wa kikao hicho Mha, Kasekenya amewataka watumishi wa bodi hiyo kuacha kufanya kazi kwa mazoea kwani mazingira ya utendaji wa taasisi ni kutoa huduma kwa watalaam wa fani ya wabunifu majengo na wakadiriaji wa majenzi.
Aidha Naibu Waziri wa ujenzi Mteule, Mha Godfrey Kasekenya, amesema Serikali inathamini mchango wa AQRB na inahitaji michango ya bodi katika kuwezesha na kuendelea ujenzi wa Tanzania ya viwanda kwa kusisitiza kuwepo kwa mafunzo ya kuwajengea uwezo wataalamu wake ili wapate uzoefu na ujuzi hatimaye waweze kushindana katika soko la ndani na nje ya nchi.
Kwa upande wa Naibu Katibu Mkuu, Bwa. Ludovick Nduhiye, amewapongeza AQRB kwa kuendelea kufanya vikao vya wafanyakazi na kuwataka watumishi kuhakikisha wanaeleza kwa uwazi changamoto zote wanazokutana nazo ili kuimarisha utendaji wa taasisi.
“Kama watumishi wa Ummamna wajibu mkubwa katika kuhakikisha majenzi yanafata viwango vinavyotakiwa kulingana na fani inavyotaka, kama wataalamu serikali inawategemea sana kwenye ushauri hususani katika kipindi hiki ambacho taasisi na wananchi wanajenga sana mji wa Dodoma”alisisitiza Bwa. Nduhije.
Naye Msajili wa Bodi Arch. Edwin John Nnunduma amesema dhumuni la mkutano huo ni kujadili na kufikia muafaka kwenye maamuzi yanayohusu maslahi ya watumishi na watendaji kazi wenye tija kwa maendeleo ya bodi na taifa.
No comments:
Post a Comment