TAARIFA YA UTEKELEZAJI WA AJENDA YA TAIFA YA KUWEKEZA KATIKA AFYA NA MAENDELEO YA VIJANA - THE HABARII

ASAS GROUP

Habari Mpya


Monday 7 August 2023

TAARIFA YA UTEKELEZAJI WA AJENDA YA TAIFA YA KUWEKEZA KATIKA AFYA NA MAENDELEO YA VIJANA

Kaimu Katibu Mkuu Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum Everline Makalla akifungua kikao cha Wakurugenzi kutoka Wizara za kisekta kwa lengo la kupokea taarifa ya utekelezaji wa Ajenda ya Taifa ya Kuwekeza katika Afya na Maendeleo kwa Vijana Balehe Agosti 07,2023 jijini Dodoma.

Baadhi ya wajumbe wa Kamati Tendaji na Sekretarieti ya utekelezaji wa Ajenda ya Taifa ya Kuwekeza katika Afya na Maendeleo kwa Vijana Balehe wakifuatilia yanayoendelea katika kikao cha Wakurugenzi kutoka Wizara za kisekta kupokea taarifa ya utekelezaji, Agosti 07, 2023 jijini Dodoma.

Na WMJJWM Dodoma

WATOTO na Vijana Balehe wameaswa kutokaa kimya bali kuzungumza kuhusu masuala mbalimbali yanayowahusu ikiwemo kujiepusha na maambukizi ya VVV/UKIMWI pamoja na huduma mbalimbali muhimu ili kufikia ndoto zao.

Hayo yamebainikia jijini Dodoma Agosti 07, 2023 wakati wa kikao cha Wakurugenzi kutoka Wizara za kisekta wakiongozwa na Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsi, Wanawake na Makundi Maalum cha kupokea taarifa ya kikao cha Sekretarieti ya uratibu wa utekelezaji wa Ajenda ya Taifa ya Kuwekeza katika Afya na Maendeleo kwa Vijana Balehe.

Akizungumza katika kikao hicho Kaimu Katibu Mkuu Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum Everline Makalla amesema Ajenda ya Taifa ya Kuwekeza katika Afya na Maendeleo kwa Vijana Balehe haileti afua mpya ila inaongeza nguvu zaidi katika kuhakikisha vijana Balehe wanapata huduma zinawahusu kwa Ustawi wao.

Ameongeza kuwa kikao hicho ni muhimu kwa kuwa kinatoa taswira ya utekelezaji wa Ajenda ya Taifa ya Kuwekeza katika Afya na Maendeleo kwa Vijana Balehe ili kuwa na taarifa muhimu itakayosaidia kuwafikia Makatibu Wakuu wa Wizara za kisekta na hatimaye Mawaziri na kuwekwa katika Mipango mbalimbali ya Wizara kwa utekelezaji wake.

Kwa upande wake Mwakilishi wa Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia ambaye ni Kamishna wa Elimu nchini Dkt. Lyabwewe Mutahabwa amesema ripoti ya utekelezaji wa Ajenda ya Taifa ya Kuwekeza katika Afya na Maendeleo kwa Vijana Balehe ni muhimu ili kuona changamoto na mafanikio yake kwa ajili ya kuweka mpango mkakati wa kuboresha utekelezaji wa Ajenda hiyo muhimu kwa taifa.

Naye Mratibu wa utekelezaji wa Ajenda ya Taifa ya Kuwekeza katika Afya na Maendeleo kwa Vijana Balehe Daniel Maro, amesema kuwa lengo la kikao hicho ni kutoa taarifa ya utekelezaji wa Ajenda kwa Wakurugenzi kutoka Wizara za kisekta ili kuwa na uelewa wa pamoja kuelekea utoaji wa taarifa kwa Makatibu Wakuu na Mawaziri kuhusu utekelezaji wa Ajenda hiyo.

No comments:

Post a Comment