TUMRUDIE MUNGU ATUEPUSHE NA MAJANGA - SHEHE MOHAMED - THE HABARII

ASAS GROUP

Habari Mpya


Tuesday 23 November 2021

TUMRUDIE MUNGU ATUEPUSHE NA MAJANGA - SHEHE MOHAMED

Shehe Athuman Mohamed akizungumza wakati wa maadhimisho ya mazazi ya Mtume (SAW) Masjidi ya Tambaza.

Na Mwandishi Wetu

WAUMINI wa Kiislamu na Watanzania kwa ujumla wametakiwa kumrudia Mungu ili awaepushe na majanga yanayolisibu Taifa na Dunia kwa ujumla.

Akizungumza katika maadhimisho ya kuzaliwa kwa Mtume (SWA), Imamu Mkuu wa msikiti wa Tambaza Shehe Athuman Mohamed alisema Tanzania na Dunia kwa ujumla inapitia kipindi kigumu sababu ni kumuacha Mungu.

“Tunapoadhimisha mazazi ya Mtume ni lazima tujirudi nakujitathimini wapi tumekosea tutubu, tufanye dua atuondolee balaa ambalo linalikumbaTaifa, ikiwemo ukame, Covid 19 na mengineyo, tukitubu na kuomba yote yanakwisha,” alisema.

Shehe Mohamed alisema siku hiyo huadhimishwa zaidi kwakupokkea mawaidha ya mtume, kusifu, kuombea amani ya nchi na dunia kwani Mtume kila alipokwenda alihubiri amani.

Aidha Shehe Mohamed aliwataka vijana kutojihusisha na vitendo vya uvunjifu wa amani ikwemo wizi, matumizi mabaya ya mtandao, kutumiwa vibaya na baadhi ya wanasiasa wasiolitakia mema Taifa na badala yake wamuunge Rais Samia Suluhu Hassan kwakuchapa kazi ili kujiletea maendeleo.

“Kama kuna kundi lolote duniani hutegemewa zaidi katika kuliletea Taifa maendeleo vijana ni injini inayotegemewa, lakini wakitumiwa vibaya basi uasi, uhasama na machafuko ni rahisi kutokea”alisema, vijana wajikite zaidi kwenye uzalishaji mali nakumrudia Mungu,” alisema.

Hata hivyo Shehe Mohamed aliihakikishia serikali kuwa Msikiti wa Tambaza na BAKWATA kwa ujumla wanafanya kazi bega kwa bega kuhakikisha amani inapatikana katika Taifa hili kwa minajili yakukemea uovu ikibidi hata kuwafichuwa waovu.

“Hatupo tayari kuona amani ya nchi hii inavurugwa, kama viongozi wa dini tutapaza sauti zetu katika kukemea uovu na uhalifu kupitia majukwaa yetu ya ibada, lakini pia niwakumbushe wananchi kushiriki sensa ya mwakani kwani pasipo kuhesabiwa tutakwamisha mipango na mendeleo yetu wenyewe,” alisema.

Kwaupande wake msaidizi wa Maalimu Badrusalum Omary alisema maadhimisho hayo ni muhimu kwani hakuna wakuenziwa kama Mtume na wanaadhimisha kwa sababu ya mazuri waliyotendewa na Mtume.

“Katika maadhimisho haya kikubwa ni kukumbushana kuwa wanyenyekevu, waadirifu na kuombeana dua zenye heri na kutoa misamaha nakupokea misamaha kwani Mtume alikuwa mwingi wa rehema na mwenye kusamehe zaidi sisi ninani hadi tusisamehe,” alisema.

Hata hivyo Maalim Omary anawataka wazazi kuwa karibu na Watoto wao ili kujua nini wanafanya wawapo mtaani na nini wanfanyiwa na pia kushirikisha viongozi wa dini pindi zinapotokea changamoto za kinidhamu ili viongozi wadini wawasaidie wazazi katika malezi bora.

Naye muumini wa msikiti huo ambaye pia ni mwanafunzi wa Chuo cha Usimamizi wa Fedha (IFM) anayesoma Shahada ya kwanza ya Uhasibu Aljabir Nzali aliwataka vijana wenzake na jamii kwa ujumla kumrudia Mola kwani ndiyo kila kitu.

“Nimefika hapa nilipo mwaka wa tatu sasa sisi jambo rahisi, lakini si kwa uwezo wangu, walimu na wahadhiri au wazazi bali ni kwa uwezo wa Mola hivyo tumrudie yeye ndiye kila kitu katika Maisha yetu.


No comments:

Post a Comment