AGREY MWANRI AKUMBUKWA UFUNGUZI WA KANISA CHAMWINO IKULU - THE HABARII

ASAS GROUP

Habari Mpya


Sunday 21 November 2021

AGREY MWANRI AKUMBUKWA UFUNGUZI WA KANISA CHAMWINO IKULU

 AGREY MWANRI AKUMBUKWA UFUNGUZI WA KANISA CHAMWINO IKULU

Baba Askofu Amoni Kinyunyu akizinduwa Kanisa Jipya la KKKT Usharika wa Chamwino Ikulu, Mtaa wa Nazareti-Buigiri wilayani Chamwino mkoani Dodoma.

Na Adeladius Makwega, Chamwino-Ikulu

KANISA la Kiinjili la Kilurtheri Tanzania (KKKT) Dayosisi ya Dodoma limefaya uzinduzi wa kanisa lake Jipya la Usharika wa Chamwino Ikulu, Mtaa wa Nazareti-Buigiri Wilayani Chamwino Mkoani Dodoma ambalo limegharimu zaidi ya shilingi za Kitanzania milioni 300.

Uzinduzi huo umefanyika Jumapili ya Novemba 21, 2021 ambapo Baba Askofu Amoni Kinyunyu aliongoza Ibada ya ufunguzi wa Kanisa hilo la kisasa likijengwa kwa michango ya washirika mbalimbali wanaosali kanisani hapo ambapo ujenzi ulianza Disemba 4, 2011.

Ibada ya ufungulizi ilianza kwa washirika kulizunguka kanisa hilo jipya mara tatu huku wakiongozwa na msalaba mbele uliobebwa na Mwinjilisti Rizikiel Shekivuli na washiriki wote wakifuata na mwisho Baba Askofu Kinyunyu.

Akizungumza katika ibada hiyo Baba Askofu Kinyunyu amesema kuwa anawapongeza sana kwa kujenga nyumba hiyo ya ibada kwa manufaa ya kiroho ya Wanausharika na Wana dayosisi.

“Ni jambo jema kushiriki katika ujenzi wa nyumba za ibada, jambo hili wale wote walioshiriki tunapaswa kuwapongeza sana wale waliopo leo na hata wale ambao hawapo kwa siku ya leo ya ushuhuda”

Baba Askofu aliongeza kuwa anawataka wakristu wote kuishi maisha mema na kutokuwa na mifarakano popote pale walipo ili maisha ya wanadamu yawe mema iwe safarini, kazini au katika shughuli zingine zozote zile.

“Anayekula nguruwe hula nyama yote bila ya kuacha chochoche lakini alae ng’ombe hula nyama lakini lazima ataacha ngozi, kwato na vinginevyo ambavyo itakuwa alama kuwa alikula nyama ya mnyama huyu, kwa hiyo maisha yetu yawe kama ya yule alae nyama ya ng’ombe na kuacha alama kwa wenzake, alama hizo ni kama ujenzi wa kanisa hili.”

Awali akisoma risala kwa baba askofu namna walivyojenga jengo hilo Mwinjilist Shekivuli alisema. 

“Sisi kama ushariki huu tuwashukuru sana washirika mbalimbali kwa kuchangia ujenzi wa kanisa letu huku hasa hasa Mheshimwa Agrey Mwanri ambaye alikuwa Naibu Waziri wa TAMISEMI wakati huo ambaye alisaidia katika michango na hata kuongezea eneo la usharika.”

Ibada hiyo ilihusisha kwaya tano ikiwamo Kwaya Kuu–Kutoka Kanisa Kuu, Kwaya Kutoka Chinangali, Kwaya Kutoka Mkuhungu, Kwaya kutoka Kanisa la Anglikani Chamwino Ikulu tangu ibada ya ufunguzi hadi ibada ya siku ya Bwana ambazo zote ziliongozwa na Askofu Kinyunyu.


No comments:

Post a Comment