SERIKALI KUJENGA MADARAJA YA MALAGARASI-ILAGALA NA LUGONESI - THE HABARII

ASAS GROUP

Habari Mpya


Saturday 30 September 2023

SERIKALI KUJENGA MADARAJA YA MALAGARASI-ILAGALA NA LUGONESI

Naibu Waziri wa Ujenzi Eng. Godfrey Kasekenya akisisitiza jambo kwa wananchi wa kata ya Kalya alipozungumza nao alipokagua maendeleo ya uanzishwaji wa barabara ya Simbo-Kalya KM 235 mkoani Kigoma.



Mbunge wa Kigoma Kusini Mhe. Nashon Bidyanguze akifafanua jambo kwa Naibu Waziri wa Ujenzi Eng. Godfrey Kasekenya alipokagua barabara ya Simbo-Kalya KM 235 mkoani Kigoma.


SERIKALI imesema katika mkakati wake wa kuufungua mwambao wa ziwa Tanganyika itajenga madaraja ya Malagarasi-Ilagala na Lugonesi ili kuunganisha kwa njia fupi mikoa ya Kigoma na Katavi na hivyo kuchochea shughuli za uzalishaji wa mazao, uvuvi na ufugaji katika maeneo hayo.

Hayo yamesemwa na Naibu Waziri wa Ujenzi Eng. Godfrey Kasekenya alipokagua maendeleo ya uanzishwaji wa barabara mpya ya Simbo-Kalya  KM 235 inayopita pembezoni mwa ziwa Tanganyika na kuunganisha mikoa ya Kigoma na Katavi.

“ Hadi mwezi Disemba tutahakikisha upembuzi yakinifu na usanifu wa kina umekamilika ili kazi ya ujenzi wa madaraja haya mawili pamoja na barabara unganishi zenye zaidi ya KM 7 uanze”, amesema Eng. Kasekenya.

Amebainisha kuwa wakati Serikali ikitafuta fedha za kuijenga barabara hiyo itahakikisha maeneo korofi yanajengwa kwa kiwango cha zege ili kuiwezesha kupitika kipindi chote cha mwaka.

Naibu Waziri huyo amewapongeza mameneja wa Wakala wa Barabara TANROADS mkoa wa Kigoma na Katavi kwa kazi za kuanzisha barabara mpya katika maeneo yao ili kurahisisha huduma ya usafiri ikiwa ni pamoja na kuunganisha barabara na bandari za ziwa Tanganyika.

 “Kwa kweli nimeridhika kwa bidii na ubunifu wa mameneja hawa ya kuanzisha barabara mpya huu ni ubunifu mzuri na Serikali itatafuta fedha ili barabara hizi zijengwe kwa lami”, amesisitiza Eng. Kasekenya.

Naibu Waziri huyo amewataka wananchi wa mikoa ya Kigoma na Katavi kulinda miundombinu ya barabara ili idumu kwa muda mrefu na kuepusha hasara kwa serikali na ukosefu wa usalama kwa wananchi wanaotumia barabara hizo.

“Acheni kuchimba mchanga barabarani na chini ya madaraja, epukeni wizi wa alama za barabarani na taa, eleweni Serikali inatumia gharama kubwa kujenga miundombinu hii hivyo kuilinda ni kuiunga mkono Serikali”, amesisitiza Eng. Kasekenya.

Meneja wa (TANROADS), mkoa wa Kigoma Eng. Narcis Choma amesema ujenzi wa barabara na madaraja utaendana na utoaji elimu ya uzalendo kwa wananchi namna ya kuilinda miundombinu kwa maslahi mapana ya taifa.

 

No comments:

Post a Comment