MAKAMU wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Philip Isidor Mpango amekutana na Diaspora wa Tanzania waliopo katika miji ya New York, Connect Cut na New Jesry nchini Marekani na kuwasihi kuendelea kuchangia maendeleo ya nchi yao.
Dkt. Mpango ametoa rai hiyo Jijini New York alipokutana kwa mazungumzo na viongozi pamoja na wanajumuiya ya wanadiaspora hao Jijini New York tarehe 18 Septemba 2022.Mhe. Dkt. Mpango amesema kitendo cha wanaDiaspora hao na wengine walioko duniani kote kujishughulisha na shughuli za uwekezaji nchini kinaendeleza jitihada za serikali za kujikwamua kiuchumi na kuleta maendeleo ya kweli kwa wananchi wake.
''Muendelee kujishughulisha na shughuli za uwekezaji nchini kwani kufanya hivyo mnachangia maendeleo ya nchi yenu, mnaiunga mkono Serikali katika jitihada za kuleta maendeleo kwa watu wake," alisema Mhe. Dkt. Mpango.
Dkt. Mpango pia amewasihi wanadiaspora hao kufuatilia na kutumia fursa mbalimbali zilizopo nchini kwa manufaa yao binafsi, ndugu na jamaa na Taifa lao kwa ujumla.
Pamoja na mambo mengine, Dkt. Mpango amewataka wanadiaspora hao kuendelea kutafuta na kushawishi wawekezaji wengi kuja nchini na kutafuta masoko ya bidhaa mbalimbali zinazopatikana nchini na kuendelea kuisemea vizuri nchi yao ya Tanzania.
Amewapongeza Diaspora wa Tanzania kwa kuendelea kutoa mchango mkubwa wa uwekezaji hasa kupitia mfuko wa UTT Amis ambapo aliasema kuwa hadi kufikia mwaka 2021 wanadiaspora wa Tanzania walikuwa wamewekeza zaidi ya Shilingi bilioni 3.9 za kitanzania katika mfuko huo.


No comments:
Post a Comment