SURA ya Bajeti kwa mwaka 2022/23 inaonesha kuwa jumla ya shilingi trilioni 41.48 zinatarajiwa kukusanywa na kutumika. Jumla ya mapato ya ndani yanatarajiwa kuwa shilingi trilioni 28.02, sawa na asilimia 67.5 ya bajeti yote.
Kati ya mapato hayo, mapato yatakayokusanywa na Mamlaka ya Mapato Tanzania yanakadiriwa kuwa shilingi trilioni 23.65 na mapato yasiyo ya kodi (Wizara, Idara, Taasisi na Mamlaka za Serikali za Mitaa) yanakadiriwa kuwa shilingi trilioni 4.37.
Misaada na mikopo nafuu kutoka kwa Washirika wa Maendeleo inatarajiwa kuwa shilingi trilioni 4.65, sawa na asilimia 11.2 ya bajeti yote.
Aidha, Serikali inatarajia kukopa shilingi trilioni 5.78 kutoka soko la ndani ambapo shilingi trilioni 3.30 ni kwa ajili ya kulipia hatifungani na dhamana za Serikali zinazoiva na kiasi cha shilingi trilioni 2.48 ni kwa ajili ya kugharamia miradi ya maendeleo.
Vilevile, Serikali inatarajia kukopa shilingi trilioni 3.03 kutoka soko la nje kwa masharti ya kibiashara kwa lengo la kuongeza kasi ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo.

No comments:
Post a Comment