DKT. NDUMBARO AZINDUA UTAFITI WA UTALII WA NDANI NA MCHANGO KWA UCHUMI - THE HABARII

ASAS GROUP

Habari Mpya


Sunday 16 January 2022

DKT. NDUMBARO AZINDUA UTAFITI WA UTALII WA NDANI NA MCHANGO KWA UCHUMI

Waziri wa Maliasili na Utalii, Dkt. Damas Ndumbaro (katikati) akiwa Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Mary Masanja ( wa kwanza kushoto) wakiwa wamenyanyua mwongozo  utakaosaidia kufanyika kwa Utalii wa ndani na mchango wa sekta hiyo  katika uchumi wa nchi kupitia mpango wa Maendeleo kwa ustawi wa Taifa na mapambano dhidi ya UVIKO 19, Wa pili kushoto ni  Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu Huria, Prof. Deus Ndaruko.

WAZIRI wa Maliasili na Utalii,  Dkt. Damas Ndumbaro amezindua rasmi utafiti wa Utalii wa ndani na mchango wa sekta hiyo  katika uchumi wa nchi kupitia mpango wa Maendeleo kwa ustawi wa Taifa na mapambano dhidi ya UVIKO 19.

 Tukio hilo la kihistoria ni la kwanza kufanyika hapa nchini na kufanywa na Wizara ya Maliasili na Utalii katika ustawi wa ukuaji wa uchumi wa nchi.

 Akizungumza wakati wa uzinduzi huo kwa kushirikiana na Chuo Kikuu Huria cha Tanzania, Waziri Dkt. Ndumbaro ameeleza kuwa, Kaya zaidi ya 3800 zinaenda kufikiwa katika utafiti huo.

‘’Mpango tunaozindua leo ni mpango muhimu sana,Kuhusiana na utalii wa ndani jambo hili halijawahi kufanyika toka tumepata uhuru, hakika ugonjwa wa UVIKO 19 umetoa darasa.

 Aidha, Dkt. Ndumbaro alimpongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mh. Samia Suluhu Hassan  kwa kuwezesha kutoa mgao wa zaidi ya Bilioni 90 ilikusaidia Wizara hiyo.

  "Rais wetu amfikilia tija zaidi na kutoa fedha hizi zaidi ya bilion 90 kwani alikuwa na uwezo wa kununulia vifaa vya kujikinga na UVIKO 19, lakini ameonelea kuzipeleka kwenye maendeleo.

 Mimi binafsi, Naibu waziri na katibu mkuuu na Naibu Katibu tumempendezesha na ametuona tuendelee kumalizia jambo lililobakia hivyo hatuta mwangusha tunaahidi kufanya kazi kwa ukubwa zaidi.’’ Alisema Dkt. Ndumbaro.

 Ambapo pia amekipongeza Chuo kikuu Huria kwa kukubari kufanya kazi hiyo ya utafiti kwani wana uwezo na ubobezi mkubwa na idara ya utalii iliyobobea watalaam.

 "Chuo cha watanzania wataalam watanzania. Sasa hawa wakusanya data zaidi ya 600 yaani na watalaam wengine jumla watafika 700 wataenda kuguswa na uwezeshwaji yote hii ni kwa uwezo wa mama Samia.

 Hata hivyo Waziri Dkt. Ndumbaro alibainisha kuwa, mwaka 2020-2021 Wizara hiyo iliweza kufanya vizuri na watalii wa ndani waliongezeka.

 ‘’Mwaka 2021 tuliweza kupata watalii wa ndani Laki saba na watalii wa nje ni  Laki Tisa ili ni ongezeko kubwa na hata Shirika la Utalii Duniani lilitupongeza kwa hatua hii kubwa licha ya changamoto ya UVIKO.

 Aidha, aliwataka Chuo kikuu huria kuzingatia fursa hiyo kwani ni kubwa kuwahi kutokea.

 "Utafit huu unaenda kutupatia takwimu na ushauri. Kuna maeneo hasa ya utalii wa ndani tunapaswa tufikie kwani  tunaenda kuongeza ajira na pia kuongeza watalii wakati wa ‘low season’ lakini pia utafiti huu utaenda kuimarisha fursa mbalimbali.’’ Alisema Waziri Dkt. Ndumbaro.

 Aidha amepongeza mkakati wa ushirikishwaji wa wadau mbalimbali,wakiwemo kushirikishwa kwa Benki kuu ya Tanzania,NBS, Uhamiaji  pamoja na Kamisheni ya utalii wa Zanzibar kwani utafiti huo unatarajiwa kufanyika Bara na Visiwani lakini pia Wadau wa ndani na nje ya Tanzania.

 ‘’Naomba sana, hii ni historia katika nchi yetu. Naziomba sana taasisi zote zitakazoshiriki  asilimia kubwa ya washiriki wawe ni vijana kwani vijana hao watadumu na watakuwa na muda mrefu na siku za baadae katika masuala haya.

Aidha, aliongeza kuwa Utafiti huu utasaidia kutengeneza dira nyingine ya miaka mitano ya wizara na kitaifa kupitia utalii lakini pia Utafiti utasaidia katika utekelezaji wa chama cha mapinduzi CCM katika kila awamu zake za miaka mitano mitano.

 "Kila mmoja awajibike kutengeneza wajibu wake na matumizi ya fedha yatumike kwa usahihi na usawa pasipokuleta chengachenga.

Naye Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Mary Masanja amesema utafiti huo utatoa dira ya mwenendo wa utalii wa ndani.

“Utalii wa ndani ni eneo pana sana ambalo tuliliacha nyuma kwa hivyo leo tunaenda kuzindua utafiti huu kwa lengo la kujua tulipotoka, tulipo na tunapoenda ili utalii wa ndani ukue”

Kwa upande wake Naibu Katibu Mkuu, Wizara ya Maliasili na Utalii, Juma Mkomi amesema Utafiti huu utawezesha sio tu kupatikana kwa takwimu sahihi bali utatoa fursa ya kujua pengo lililopo kati ya utalii wa ndani na wa nje.

 Serikali imefikia uamuzi wa kufanya utafiti huo kwa sababu sekta ya utalii imekuwa ikichangia katika uchumi wa nchi zaidi ya Shilingi trilioni 6.06 (Dola za Marekani Bilioni 2.6) na kuzalisha ajira takriban milioni 1.5 (za moja kwa moja na zisizo za moja kwa moja).

 Kwa sasa kila kona ni gumza juu ya Royal tour aliyofanya Rais  wetu, duniani kote. Rais wetu anapenda utalii…"Piga ua, lazima Rais 2025 arudi madarakani." Alisema Waziri Dkt.Ndumbaro.

 Kwa upande wake, Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu Huria, Prof. Deus Ndaruko  amesema mradi unatarajia kuanza hivi karibuni na utakuwa wa miezi minne ambapo anahakika utakuwa utafiti mkubwa na mzuri.

‘’Tunashukuru Wizara ya Maliasili kwa ushirikiano huu na tunaahidi kuzitumia vizuri fedha  na watanzania wataiona wizara wakitembea katika maeneo yao mbalimbali.’’ Alisema Prof. Ndaruko.

No comments:

Post a Comment