DK ZAINABU CHAULA AAGIZA VITUO VYA MAWASILIANO ZANZIBAR KUJIENDESHA KWA FAIDA - THE HABARII

ASAS GROUP

Habari Mpya


Thursday 2 July 2020

DK ZAINABU CHAULA AAGIZA VITUO VYA MAWASILIANO ZANZIBAR KUJIENDESHA KWA FAIDA


Katibu Mkuu wa Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano (Sekta ya Mawasiliano) wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Zainabu Chaula (wa kwanza kushoto) akimsikiliza Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Ujenzi Mawasiliano na Usafirishaji wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ), Bw. Shomari Omar (hayupo pichani) kabla ya kuanza ziara ya kukagua vituo vya TEHAMA visiwani Zanzibar. Kulia kwake ni Naibu Katibu Mkuu Sekta ya Mawasiliano Dk. Jim Yonazi.

Kituo cha TEHAMA cha Mkokotoni kilichopo Unguja, moja ya vituo sita vya TEHAMA vilivyokaguliwa na Katibu Mkuu wa Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano (Sekta ya Mawasiliano), Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk. Zainabu Chaula kisiwani Zanzibar.


Na Faraja Mpina, Zanzibar


KATIBU Mkuu Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano (Sekta ya Mawasiliano) wa Jamhuri nya Muungano ya Tanzania, Dkt. Zainabu Chaula ameelekeza kuwa vituo vya TEHAMA vilivyojengwa Zanzibar na Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote nchini (UCSAF) kujiendesha kibiashara badala ya kutoa huduma bure kwa wananchi, ili kuweza kumudu gharama za uendeshaji ikiwa ni pamoja na kuleta faida kwa Serikali.


Dkt. Chaula aliyasema hayo mwanzoni mwa wiki hii alipokuwa katika ziara yake ya kwanza ya kikazi visiwani Zanzibar kukagua  vituo 10 vya TEHAMA  vilivyojengwa na Mfuko wa Mawasiliano kwa wote nchini UCSAF. Vituo hivyo viko 10 Unguja vituo 4 viko Pemba. 


“Tusiwe waumini wa vitu vya bure, dhumuni la Serikali kufanya uwekezaji huu sio kupata hasara ila ni kusogeza huduma kwa wananchi kwa matarajio ya uwekezaji huo utaweza pia kujiendesha, kufanya maboresho na kuleta faida kwa Serikali”, alisema Dkt. Chaula kwa msisitizo.  


Aidha Dk.t Chaula amewataka Shirika la Mawasiliano Tanzania (TTCL) pamoja na Shirika la Posta (TPC) kuwa wabunifu kwa kuweka huduma zao katika vituo hivyo vya TEHAMA kama vile miamala ya T-Pesa, kuuza vocha na laini za simu pamoja na huduma za Posta mtandao huku akiwaasa wataalamu kutumia taaluma zao  kuwashauri vizuri viongozi katika maeneo yao ya kazi.


Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Ujenzi, na Usafirishaji-Serikali ya Mapinduzi Zanzibar bwana Shomari Omar, amekiri kuwa Dkt Chaula amewafumbua macho kwasababu hapo awali hawakuwa na mtazamo wa kibiashara katika matumizi ya vituo hivyo vya TEHAMA ambavyo vimejengwa kwa gharama kubwa na Serikali.

“Iwapo vituo hivi vitatoa huduma bora za mawasiliano na intaneti yenye kasi kubwa, wananchi watakuwa tayari kutumia na kulipia gharama za huduma hiyo, hii itasaidia kupoteza kabisa dhana ya kuviendesha vituo hivi kwa hasara”, alisema Bwana Omar.


Nae Meneja wa TCRA Ofisi ya Zanzibar, Esuvatie Massinga amesema kuwa Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) ndio msimamizi na mdhibiti wa Mawasiliano na wanajipanga kuhakikisha wanaweka programu maalum zitakazozuia wanafunzi na wateja kuangalia picha za ngono ikiwa ni pamoja na kuhakikisha kuwa vituo hivyo havitatumiwa kuvunja sheria za matumizi salama ya mtandao.


Mtendaji Mkuu wa Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote nchini (UCSAF) Bi. Justina Mashiba ametoa taarifa mbele ya ujumbe wa Katibu Mkuu kuwa gharama za ujenzi wa kituo kimoja cha TEHAMA umegharimu kiasi cha shilingi milioni 113 na makadirio ni kituo kimoja kuingiza faida ya zaidi ya shilingi milioni sita kwa mwaka iwapo vitasimamiwa vizuri na waendeshaji wa vituo vivyo vya kisasa vya mawasiliano.

Katibu Mkuu wa Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Sekta ya Mawasiliano wa Serikali ya Muungano ameongozana na Naibu Katibu Mkuu wa Sekta ya Mawasiliano Dkt. Jim Yonazi, Mkurugenzi wa Huduma za Mawasiliano injinia Clarence Ichekweleza na Mkurugenzi wa Rasilimali Watu Bibi Kitolina Kippa.

Wengine katika msafara wa Katibu Mkuu wa kukagua vituo hivyo vya TEHAMA Zanzibar ni pamoja na Mtendaji Mkuu wa Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote nchini Bi. Justina Mashiba, Kaimu Mkuu wa Manunuzi bibi Lightness Makundi, Mwanasheria Eunice Masigati wa Wizara ya Ujenzi, uchukuzi na Mawasiliano (Sekta ya Mawasiliano) pamoja na watumishi wengine wa Wizara na Mfuko wa mawasiliano kwa Wote.

No comments:

Post a Comment