CORONAVIRUS: KIFO CHA KWANZA CHATHIBITISHWA MAREKANI JIMBO LA WASHINGTON - THE HABARII

ASAS GROUP

Habari Mpya


Sunday 1 March 2020

CORONAVIRUS: KIFO CHA KWANZA CHATHIBITISHWA MAREKANI JIMBO LA WASHINGTON


Kuna uwezekano mkubwa wa kutokea kwa visa vingi zaidi vya coronavirus

MAREKANI yathibitisha kisa cha kwanza cha ugonjwa wa coronavirus katika jimbo la Washington.

Maafisa wamesema kwamba mgonjwa huyo, 50, alikuwa mwanaume ambaye hali yake ya afya haikuwa nzuri.

Rais Donald Trump amesema kwamba visa vingi zaidi vinatarajiwa kutokea na akaongeza kuwa nchi hiyo imejitayarisha kwa lolote litakalo tokea.

Jumapili, Australia na Thailand pia zimerekodi kifo cha kwanza cha coronavirus.

Mwanamume wa miaka 78 wa Australia aliaga dunia baada ya kuambukizwa ugonjwa huo katika meli ya Diamond Princess nchini Japani mwezi uliopita.

Thailanda ambayo imethibitisha visa 42 vya coronavirus inasema mwanaume wa miaka 35, aliyekufa pia alikuwa anaugua homa ya dengue.

Zaidi ya visa 85,000 vya ugonjwa wa coronavirus vimethibitishwa katika nchi 57 kote duniani huku vifo 3,000 vikithibitishwa, kulingana na Shirika la Afya Duniani.

Idadi kubwa ya vifo hivyo ni kutoka China ambapo virusi hivyo vilianzia mwishoni mwaka jana.

Kipi kinachoendelea Marekani?

Maafisa wa afya wa eneo wamethibitisha Jumamosi kwamba mwanaume huyo alikufa katika kaunti ya King jimbo la Washington. Na kuongeza kwamba hakuwa amesafiri katika maeneo yalio kwenye hatari ya kupata ugonjwa huo.

Gavana wa jimbo la Washington, Jay Inslee, ametangaza hali ya hatari kama hatua alioichukua baada ya kutokea kwa kisa hicho kipya katika jimbo lake.

Hilo linatokea wakati maafisa katika pwani ya magharibi ya Marekani - California, Oregon na Washington - wakiwa na wasiwasi kuhusu visa vinavyowatokea wagonjwa ambao hawakuwa wametembelea eneo lenye mlipuko ama kutangamana na yeyote aliyekuwa na ugonjwa huo.


Visa viwili vya coronavirus vimethibitishwa Washington
Maafisa wa jimbo la Washington Jumamosi wamesema wanachunguza uwezekano wa kutokea kwa mlipuko wa coronavirus katika makao ya kuwatunza wazee.

Dr Jeffrey Duchin, afisa wa afya eneo la Seattle, amesema kuna visa viwili vyenye kuhusishwa na makao ya kuwatunza wazee, mhudumu mmoja wa afya na mkaazi mwenye umri wa miaka 70.

Dr Duchin amesema kuwa wakazi 27 na wahudumu 25 katika kituo hicho walionyesha dalili kama hizo. Aidha maafisa wamesema visa zaidi vya coronavirus vinatarajiwa.

Hadi kufikia sasa, WHO imesema visa 62 vimeripotiwa nchini Marekani.

Raia wa Marekani alikufa Uchina mji wa Wuhan, kitovu cha virusi hivyo.

Marekani inachukua hatua gani?

Huku akikiri kuwa visa vingi zaidi vinatarajiwa, Rais Trump amesema kwamba hakuna haja ya kuingiwa na hofu juu ya mlipuko huo.

Makamu rais Mike Pence pia alitangaza kwamba marufuku inayoendelea ya kusafiri kutoka Iran imepanuliwa na sasa inajumuisha raia yeyote wa kigeni ambaye ametembelea nchi hiyo ndani ya siku 14.

Mbali na China, Iran imerekodi idadi kubwa ya vifo kwasababu ya coronavirus.

Pia alitaka raia wasitembelee nchi zilizoathiriwa na ugonjwa huo sana kama vile Italia na Korea Kusini.

Ndege za Marekani zimesema kwamba zitasitisha safari zake za kasakzini mwa Italia mji wa Milan na pia itakuwa na safari moja tu kwa siku kutoka Marekani kwenda Italia kati ya Philadelphia na Rome.

Australia yarekodi kifo cha kwanza cha Corona

Mtu wa kwanza kufa kwa virusi hivi Australia ni mwanamume kutoka Perth.

Alikuwa miongoni mwa raia 160 wa Australia kuhamishwa kutoka kwa meli ya Diamond Princess mwezi uliopita.


Watu 621 waliambukizwa virusi vya corona katika meli ya Diamond Princess nchini Japan
Mke wake, 79, ambaye pia aliambukizwa bado yuko hospitalini.

Zaidi ya watu 600 katika meli ya Diamond Princess iliyokuwa na abiria 3,700 waliambukizwa virusi hivyo wakiwa kwenye meli hiyo ambayo imekuwa kwa karantini katika pwani ya Japani bandari ya Yokohama tangu mwanzoni mwa Februari.

Jumamosi mwanaume raia wa Uingereza ambaye pia alikuwa kwenye meli hiyo ndo raia wa kwanza wa Uingereza na abiria wa sita kutoka kwa meli hiyo kuaga dunia kwasababu ya kuambukizwa coronavirus (Covid-19).

Kipi kinachotokea katika maeneo mengine?

Jumapili, visa vingine vipya 573 vya coronavirus vimethibitishwa China ikiwa ni ongezeko la juu zaidi kila siku kwa wiki nzima. Idadi ya hivi karibuni ya maambukizi imefikia 79,824.

Vifo 35 pia vimethibitishwa nchini China vyote isipokuwa kimoja tu, vikiwa vimetokea eneo lililoathirika zaidi la Hubei.
Kando na China, Korea Kusini imeripoti visa vingine 376 vya ugonjwa huo nchini humo na kufikisha jumla ya maambukizi zaidi ya 3,500.

Wakati huohuo, Ufransa imepiga marufuku mikusanyiko yoyote ya zaidi ya watu 5,000 kama sehemu ya kujaribu kudhibiti mlipuko huo.

Idadi jumla ya visa vipya vya corona nchini Ufaransa imeongezeka hadi 100 Jumamosi. Wagonjwa wawili wameaga dunia.

Ecuador na Qatar zimekuwa nchi za hivi karibuni zaidi kutangaza kuthibitisha visa vya kwanza vya coronavirus.

-BBC

No comments:

Post a Comment