WAGANGA WAKUU WA MIKOA WAPEWA SIKU 30 KUTATHMINI UTENDAJI WA KAMATI ZA AFYA MIKOA, WILAYA - THE HABARII

ASAS GROUP

Habari Mpya


Monday 6 May 2019

WAGANGA WAKUU WA MIKOA WAPEWA SIKU 30 KUTATHMINI UTENDAJI WA KAMATI ZA AFYA MIKOA, WILAYA


Naibu Katibu Mkuu OR-TAMISEMI (Afya), Dk. Dorothy Gwajima akiongea na wajumbe wa kamati za usimamizi huduma za Afya mkoa na wilaya za Namtumbo, Songea na Songea Manispaa katika ukumbi wa Ofisi ya Mkuu wa Wilaya ya Songea.

Naibu Katibu Mkuu OR-TAMISEMI (Afya) Dk. Dorothy Gwajima wa kwanza kulia akiongea na ndugu wa wagonjwa kusikiliza kero zao alipotembelea na kukagua kituo cha Afya Mjimwema Manispaa ya Songea.


WAGANGA wakuu wa Mikoa Tanzania Bara wamepewa mwezi mmoja kuhakikisha kuwa wanazifanyia tathmini ya kina kamati za Uendeshaji Huduma za Afya za Mikoa na wilaya zao kuona kama zinaendana na kasi ya mabadiliko yanayokusudiwa na Serikali ya awamu ya tano.

Agizo hilo limetolewa jana mjini Songea na Naibu Katibu Mkuu Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, TAMISEMI anayeshughulikia Afya Dk. Dorothy Gwajima wakati akizungumza  na wajumbe wa kamati ya Uendeshaji Huduma za Afya ya Mkoa wa Ruvuma pamoja za Halmashauri za wilaya ya  Namtumbo na Songea pamoja na Manispaa ya Songea.

Amesema anawapa siku 30 Waganga wakuu wa Mikoa yote kuhakikisha kuwa wanafanya tathmini ya wajumbe waliopo katika ofisi zao kama wanatosha kuendelea na nyadhifa zao za kusimamia jukumu la uendeshaji huduma za afya katika mikoa na halmashauri zao.

Dk. Gwajima ameongeza kuwa endapo itabainika kuwa baadhi ya wajumbe wa kamati hizo hawana sifa zinazowafanya kushindwa kutekeleza majukumu yao ya usimamizi na uendeshaji huduma za afya katika maeneo yao, waganga wakuu wa mikoa watalazimika kuwaweka pembeni wajumbe hao na kuunda upya kamati ambazo zitaweza kuiendeleza agenda ya mabadiliko katika sekta ya afya.

“Kinyume na hapo katika ziara hizi ninazoendelea kuzifanya mikoani nikikuta yupo Mganga Mkuu ambaye ametulia tu, mapungufu katika vituo bado yapo na amewezeshwa na serikali, ajue wazi kuwa wa kutoka wa kwanza atakuwa yeye,” amesema Dk. Gwajima na kuongeza:

“Haiwezekani tukute mapungufu madogo kabisa katika vituo, ambayo yangeweza kuonwa na wao walioko huko eti hayaonekani hadi tuje sisi kutoka Tamisemi ndiyo mapungufu hao yafanyiwe kazi,” amesisitiza Dk. Gwajima.

Naibu Katibu Mkuu huyo ameonya tabia iliyojengeka miongoni mwa wajumbe wa kamati za uendeshaji huduma ya afya kukimbilia kuomba msamaha pindi zinaposhindwa kutekeleza majukumu yake kwa makusudi.

Amesema huu ni wakati wa kuboresha sekta ya afya katika vituo vya afya na zahanati kwa kuhakikisha kuwa mazingira ya utoaji huduma yanaboreshwa ili yaweze kuwavutia wananchi wengi kukimbilia kupata huduma katika zahanati na vituo vya afya vinavyomilikiwa na serikali.

Dk. Gwajima amesema kuwa kamwe hatawapa nafasi wajumbe wa kamati za uendeshaji huduma za afya wa mikoa na wilaya ambao siku zote wamekuwa ni watu wa visingizio vya kuomba kusamehewa ama kupewa muda kuwa wamefahamu mapungufu yao.

Amesema angependa kuona kamati za uendeshaji huduma za afya katika  mikoa na halmashauri zikijikita katika kuongelea mambo makubwa yanayolenga kuishirikisha sekta na serikali kuu.

“Hivi vitu vidogo vidogo vya kitaalamu tubebe sisi wenyewe, wananchi wametuunga mkono, tumeweza kushirikiana nao kujenga zahanati na vituo vya afya katika mikoa na halmashauri zetu hivyo ni jukumu letu sasa kuhakikisha kuwa tunatoa huduma bora za afya kwa wananchi,” amesema.

Kwa mujibu wa Dk. Gwajima, katika ziara zake alizokwisha zifanya katika mikoa ya Morogoro, Dodoma, Njombe na Ruvuma amejionea mapungufu mbalimbali ya utoaji wa huduma bora za afya katika vituo vya afya na zahanati.

Ameongeza kuwa mapungufu hayo ambayo ameyashuhudia kwenye vituo vya afya na zahanati zinazomilikiwa na umma yametokana na watendaji hao  kutopata usimamizi unaostahili kutoka kwa kamati za usimamizi  na uendeshaji wa huduma za afya za mikoa na halmashauri husika.

Dk. Gwajima anaamini kuwa kushindwa kwa kamati za uendeshaji ndiko kulikopelekea kukithiri kwa uchafu katika majengo ya vituo vya afya na zahanati nchini licha ya vituo hivyo kuwa na fedha za uendeshaji wake.

Sambamba na kuwataka waganga wakuu wa mikoa kuzitathmini kamati hizo, Dk. Gwajima amewataka waganga wakuu wote kutambua kuwa  Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dk. John Pombe Magufuli ana agenda moja tu ya kuleta mabadiliko katika sekta ya afya.

 “Hatutapimwa kwa idadi ya semina au vituo vya afya tulivyojenga bali kwa ubora wa kazi za kuhudumia wananchi,” amesema.

Dk. Gwajima amebainisha mapungufu kadhaa aliyoyaona kwenye ziara yake kuwa ni pamoja kuwepo kwa malalamiko toka kwa wagonjwa na  kukosekana kwa takwimu sahihi za utendaji kazi.

Akiwa katika kituo cha afya Mjimwema Manispaa ya Songea Naibu Katibu Mkuu Dk. Gwajima alipokea kero za wagonjwa kuhusu uwepo wa kauli mbaya toka kwa wauguzi na tatizo la ukosefu dawa hususan  akina mama wajawazito
“Hapa Mjimwema nimebaini kasoro nyingi mojawapo kauli mbaya za watumishi na tatizo la dawa na vifaa tiba kwa wagonjwa ” Dk. Gwajima alionya.

Kwa upande wake Mganga Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma Dk. Jairy Khanga ameahidi  kuchukua hatua za mapema kufanya mabadiliko ya utendaji kazi wa kamati za usimamizi wa huduma za afya katika mkoa wa Ruvuma .

No comments:

Post a Comment