RAIS MAGUFULI AFANYA MAZUNGUMZO NA MKURUGENZI WA IMF...! - THE HABARII

ASAS GROUP

Habari Mpya


Monday 6 May 2019

RAIS MAGUFULI AFANYA MAZUNGUMZO NA MKURUGENZI WA IMF...!

Rais Dkt. John Pombe Magufuli akiwa katika mazungumzo na Mkurugenzi wa Idara ya Afrika wa Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF) Bw. Abebe Aemro Selassie alipokutana naye Ikulu jijini Dar es salaam
leo Jumatatu Mei 6, 2019.

Rais Dkt. John Pombe Magufuli akimtambulisha  Mkurugenzi wa Idara ya Afrika wa Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF) Bw. Abebe Aemro Selassie kwa Waziri wa Fedha na Mipango Dkt. Philip Mpango na Waziri wa mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Profesa Palamagamba Kabudi alipokutana na kufanya mazungumzo naye Ikulu jijini Dar es salaam leo Jumatatu Mei 6, 2019.

RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dk. John Pombe Magufuli tarehe 06 Mei, 2019 amekutana na kufanya mazungumzo na Mkurugenzi wa Idara ya Afrika wa Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF) Bw. Abebe Aemro Selassie Ikulu Jijini Dar es Salaam.

Baada ya mazungumzo hayo Bw. Selassie amesema aliomba kukutana na Mhe. Rais Magufuli ili kuzungumzia masuala mbalimbali yanayohusu uhusiano wa muda mrefu kati ya Tanzania na IMF na jinsi shirika hilo linavyoshiriki katika kutoa ushauri wa kiuchumi.

Bw. Selassie amempongeza Mhe. Rais Magufuli na Serikali anayoiongoza kwa juhudi kubwa zinazofanywa kuwekeza katika miradi mikubwa ikiwemo miundombinu itakayopunguza gharama za nishati ya umeme.

Kuhusu kuvuja kwa taarifa za ukuaji wa uchumi, Bw. Selassie amesema IMF itatuma timu ya wataalamu wake itakayokutana na timu ya wataalamu wa Wizara ya Fedha na Mipango ya Tanzania kwa lengo la kupitia maeneo yote yaliyoanishwa katika matazamio ya ukuaji uchumi ya IMF na yale ya Serikali ya Tanzania.

“Mimi na Mhe. Rais Magufuli tumekubaliana kuwa IMF na Tanzania watabaki kuwa wadau wanaoaminiana, tunaona fursa nyingi na muhimu katika nchi hii ikiwemo mipango mizuri ambayo Mhe. Rais Magufuli ameianzisha.

Katika wiki zijazo, tutaendelea na mazungumzo na kuendelea kufanya kazi kwa ukaribu na Serikali ya Tanzania na tutaleta timu ya wataalamu watakaokuja kujadiliana na Serikali ya Tanzania ili kutazama maeneo yote yaliyofanyiwa mageuzi makubwa na kuyawianisha na ukuaji wa uchumi” amesema Bw. Selassie.

Waziri wa Fedha na Mipango Mhe. Dkt. Philip Mpango amewahakikishia Watanzania kuwa wizara yake imejipanga kutoa ufafanuzi wa maeneo yote ambayo yanapaswa kuwemo katika taarifa ya IMF ya ukuaji wa uchumi wa Tanzania ikiwemo utelezaji wa miradi mikubwa ya kiuchumi.

“Ili uchumi wa nchi ukue ni lazima uwe unawekeza, na bahati nzuri sana Mhe. Rais amemueleza mgeni wake jinsi tunavyowekeza kwenye miundombinu hususani ujenzi wa reli ya kati, jinsi tunavyowekeza katika ujenzi wa bwawa kubwa litakalotupatia megawati 2,100 za umeme na pia miradi ya barabara na viwanda vingi vilivyojengwa, haya ndio yanayokuza uchumi na sisi tunaamini kabisa wenzetu hawakuyazingatia kabisa katika taarifa ya awali (iliyovuja)” amesema Mhe. Dk. Mpango.

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Prof. Palamagamba Kabudi amewatoa shaka wawekezaji kutoka nchi mbalimbali kuendelea kuwa na imani na mazingira ya uwekezaji ya Tanzania na amewataka Watanzania kutokua na hofu kwamba wawekezaji watapungua kwani wawekezaji hao wanaendelea kuja.

“Nashukuru kwamba hata wawekezaji wenyewe hawana hofu kwani hata baada ya taarifa hiyo kuwa imevujishwa bado wengi wameendelea kuja na kuonesha nia ya kufanya kazi na sisi, na nashukuru Shirika la Fedha la Kimataifa kwa kuja kuzungumza na sisi, hiyo ni dalili kuwa shirika hili bado lipo nasi na bado tunaendelea na mazungumzo, wale ambao walidhani pana ugomvi mkubwa kati ya Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF) na Tanzania walikuwa wamekosea kabisa, na msimamo wa Tanzania utafahamika baada ya mazungumzo kuanza na kuweza kuwapitisha katika miradi mikubwa ya maendeleo ambayo inafanyika,” amesema Mhe. Prof. Kabudi.

Rais Dkt. John Pombe Magufuli akisalimiana na Mkurugenzi wa Idara ya Afrika wa Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF) Bw. mAbebe Aero Selassie alipokutana na kufanya mazungumzo naye Ikulu jijini Dar es
salaam leo Jumatatu Mei 6, 2019.

No comments:

Post a Comment