VODACOM TANZANIA WATOA MSAADA KWA WATOTO WENYE MAHITAJI MAALUM KITUO CHA MWANANGU SPECIAL MKURANGA - THE HABARII

ASAS GROUP

Habari Mpya


Thursday 7 March 2019

VODACOM TANZANIA WATOA MSAADA KWA WATOTO WENYE MAHITAJI MAALUM KITUO CHA MWANANGU SPECIAL MKURANGA

Mkuu wa Wilaya ya Mkuranga Bw. Filberto Sanga akipokea msaada uliotolewa na taasisi ya Vodacom Tanzania Foundation kutoka kwa Meneja Mawasiliano na Matukio wa kampuni ya Vodacom Tanzania, Christina Murimi (kushoto) na Meneja Mahusiano, Alex Bitekeye (kulia), kwa ajili ya kusaidia watoto wenye mahitaji maalumu wanaoshi katika kituo cha Mwanangu Special kilichopo Vikindu mkoani Pwani. Katika kusherehekea wiki ya wanawake duniani wafanyakazi wa kampuni hiyo kupitia mpango wao wa Pamoja na Vodacom wametoa vifaa vyenye thamani ya TZS 9.5m kwa watoto hao ili kuwezesha maisha yao ya kila siku na kufikia ndoto na malengo yao. Wengine ni Mkurugenzi wa kituo hicho, Walter Miya (kati) na Jennifer Shumbusho (wa pili kulia) mmoja wa wazazi wa watoto hao.


Meneja Mawasiliano na Matukio wa kampuni ya Vodacom Tanzania Christina Murimi (kushoto) akimkabidhi Mkurugenzi wa kituo cha Mwanangu Special, Walter Miya vifaa vya watoto wenye mahitaji maalumu kutoka taasisi ya Vodacom Tanzania Foundation. Akishuhudia makabidhiano hayo ni Mkuu wa Wilaya ya Mkuranga Bw. Filberto Sanga (katikati). Katika kuadhimisha wiki ya wanawake duniani wafanyakazi wa kampuni ya Vodacom Tanzania PLC kupitia mpango wao wa Pamoja na Vodacom wametoa msaada wenye thamani ya TZS 9.5m kwa watoto hao kwa lengo la kuwawezesha katika maisha yao ya kila siku ili kufikia ndoto na malengo yao.  

KATIKA kuadhimisha wiki ya wanawake duniani, wafanyazi wa kampuni ya mawasiliano ya Vodacom Tanzania Plc, kupitia mpango wake wa Pamoja na Vodacom ulio chini ya taasisi ya Vodacom Tanzania Foundation leo wamechangia vifaa mbali mbali vyenye thamani ya shilingi milioni 9.6 kwa kituo cha watoto wenye uhitaji maalum kiitwacho Mwanangu Special kilichopo Mkuranga, mkoani Pwani. Kituo hicho kina jumla ya watoto 40, kati yao 20 ni wale wenye mahitaji maalum kama vile mgongo wazi, vichwa vikubwa na down syndrome.

Wafanyakazi hao wametoa vifaa kama vile; viti maalum, magongo ya kutembelea, magongo ya kusimamia, mashine za uzito, viatu vya ‘Special Orthopedics’, vitanda vya watoto walemavu, mashine za kufulia nk. ambavyo ni mahitaji muhimu kwa watoto hao. Mbali na misaada hiyo, wafanyakazi wa Vodacom pia walijitolea muda wao kucheza na kufurahi pamoja na watoto hao kwa ajili ya kuwapatia faraja.

Mkuu wa Wilaya ya Mkuranga, Bw. Filberto Sanga aliipongeza kampuni ya Vodacom kwa mpango huo akisema “Serikali yetu imedhamiria kuboresha maisha ya kila mtanzania ili kutimiza dira ya maendeleo ya taifa na jitihada kama hizi kutoka kampuni binafsi zinasaidia serikali kutimiza malengo yake”. Bw. Sanga pia aliishukuru kampuni ya Vodacom huku akifafanua namna ambavyo msaada huo utasaidia kuhudumia watoto wenye ulemavu nchini na kuhimiza taasisi zingine kufuata nyayo za Vodacom. 

Mpango wa Pamoja na Vodacom umekuwa ukitumiwa na wafanyakazi wa kampuni hiyo ili kurejesha fadhila kwa jamii. Mpango huu umewafanya wafanyakazi wa kampuni hiyo kuwa mawakala wa mabadiliko kwa kusaidia kutatua changamoto zilizopo katika jamii.

Akizungumza wakati wa makabidhiano, Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano na Uhusiano wa Vodacom Tanzania, Bi Jacquiline Materu alisema “Wafanyakazi wa Vodacom, tunashauku ya kuisaidia jamii yetu na huu umekuwa ni utaratibu wetu kwa miaka zaidi ya 12 kupitia Vodacom Tanzania Foundation. Katika kusherehekea wiki hii ya wanawake duniani, tumeona ni vyema kusherehekea na wadogo zetu, kuwapatia mahitaji muhimu na pia kuwawezesha kuwa na nyenzo muhimu za kuwasaidia kufikia ndoto zao kwani ulemavu sio kikwazo cha mafanikio”.

No comments:

Post a Comment