WAZIRI LUKUVI, HASUNGA WASISITIZA WANANCHI KUHESHIMU - THE HABARII

ASAS GROUP

Habari Mpya


Tuesday 11 September 2018

WAZIRI LUKUVI, HASUNGA WASISITIZA WANANCHI KUHESHIMU


Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, William Lukuvi (wa pili kushoto) akisitiza msimamo wa Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Japhet Hasunga (wa pili kulia) alioutoa leo kuhusu umuhimu wa kuheshimu mipaka ya msitu wa Hifadhi ya Kazimzumbwi kwa Wananchi wanaouzunguka msitu huo katika eneo la Zingiziwa wilayani Ilala mkoani Dar es Salaam.



Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Japhet Hasunga akitoa msimamo kwa wananchi wanaozunguka Msitu wa Hifadhi wa Kazimzumbwi kuhusu umuhimu wa kuheshimu mipaka ya Hifadhi wa Misitu huo kwa ajili ya manufaa ya wananchi wote wakati alipokuwa akizungumza na wananchi hao katika eneo la Zingiziwa wilayani Ilala mkoani Dar es Salaam. 


Baadhi ya wananchi wanaozunguka Msitu wa Hifadhi wa Kazimzumbwi wa katika eneo la Zingiziwa wakifuatilia mkutano uliowakutanisha Waziri wa Ardhi na Maendeleo ya Makazi, William Lukuvi pamoja na Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Japhet Hasunga wakisisitizwa umuhimu wa kuheshimu mipaka ya Msitu wa Hifadhi wa Kazimzumbwi kwa ajili ya manufaa ya wananchi wote.

 
SERIKALI imewataka wananchi wanaoishi kuzunguka Hifadhi ya Msitu wa Kazimzumbwi waliokuwa wamefungua kesi na baadaye kushindwa waendelee kuheshimu mipaka ya Msitu huo huku Chama Cha Mapinduzi kikiangangalia namna bora ya kuwasaidia.

Hatua hiyo inakuja kufuatia Wananchi hao waliokuwa na mgogoro wa Ardhi ndani ya Msitu huo kufungua kesi mwaka 2017, kwenye Mahakama Kuu Kitengo cha Ardhi na maamuzi ya shauri la madai hayo yaliipa serikali ushindi, baada ya wananchi hao kushindwa kuonyesha ushahidi wa umiliki wa ardhi ikiwa ni ushahidi wa manunuzi na urithi wa ardhi hiyo katika Msitu wa Hifadhi ya Kazimzumbwi.

Akizungumza kwenye mkutano na wananchi katika eneo la Zingiziwa wilayani Ilala mkoani Dar es Salaam, Waziri wa Ardhi na Maendeleo ya Makazi, Wiliam Lukuvi amewaambia wananchi hao kuwa hawana haki kwenye ardhi hiyo kwa mujibu wa hukumu iliyotoka.

Aliongeza kuwa mipaka ya msitu huo ipo sahihi na si vinginevyo hali iliyopelekea wananchi hao kushindwa  kukata rufaa.

 Hata hivyo Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi William Lukuvi  amejipa siku 30 kuangalia namna ya kuwasaidia wakazi hao walioshindwa kesi.

 Ameongeza kuwa tayari ameshaunda kamati iliyopewa muda wa miezi miwili na tayari imeshamaliza mwezi mmoja na hivyo itatoa majibu ndani ya siku 30 lengo likiwa ni kuwasaidia wananchi hao ambao kisheria walishindwa kesi.

"Mgogoro huu ulishafika mahakamani na uamuzi ukatolewa kuwa mmevamia hilo lipo wazi na sisi hatupingani na uamuzi wa mahakama. Ila kwa kuwa nyie ni wananchi wetu, CCM imeamua kununua kesi, sio kwa maana ya kupinga mahakama Bali ni kwa kuangalia tunawasaidia vipi," alisema Lukuvi.

Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Japhet Hasunga amesema wizara yake haina tatizo na wakazi hao zaidi ya kuhakikisha msitu huo uko salama. Amesema katika kipindi ambacho msitu huo ulivamiwa athari kubwa zilijitokeza.

"Msitu huu tunaweza kusema ndio mapafu ya Dar, sasa ukivamiwa kwa kuwekwa Makazi au shughuli za kibinadamu mambo yanakuwa mabaya,”

Tunategemea tupate hewa nzuri kutoka huku lakini wao walivamia na kutengeneza hewa chafu. Sisi tunachosimamia ni kuhakikisha msitu unatunzwa na kubaki kuwa msitu," amesema.

Baadhi ya wawakilishi wa kundi hilo la wananchi waliokuwa wamevamia msitu huo wameeleza kuwa wanachotaka ni kuonyeshwa mipaka ya kitaalam ya unapoanzia msitu huo.

No comments:

Post a Comment