WATUMISHI WA SERIKALI WAHIMIZWA KUTEMBELEA VIVUTIO VYA UTALII - THE HABARII

THE HABARII

HABARI | MATUKIO | MICHEZO.


ASAS GROUP

Habari Mpya


Tuesday, 21 August 2018

WATUMISHI WA SERIKALI WAHIMIZWA KUTEMBELEA VIVUTIO VYA UTALII


1.    Mkurugenzi wa  Utawala na Rasilimali Watu wa Wizara ya Maliasili na Utalii, Bw. Lusius Mwenda (kushoto) akiwa ameongoza na Watumishi zaidi ya 50 wa Wizara hiyo wakipanda kilima kwenda kuangalia michoro ya miambani katika kituo cha Utalii cha Kolo  kilichopo wilayani Kondoa mkoani Dodoma jana ikiwa lengo la ziara hiyo ni kuhamasisha utalii wa ndani kwa Watumishi wa Serikali. Wa pili ni Mkuu wa Kituo cha Kolo, Zuberi Mabie. 



1.    Mkuu wa Kituo cha Utalii, Kolo chenye michoro ya miambani, Zuberi Mabie akiwa na watumishi wa Wizara ya Maliasili na Utalii akiwaonesha michoro ya miambani katika kituo cha Utalii cha Kolo  kilichopo wilayani Kondoa mkoani Dodoma jana ikiwa lengo la ziara hiyo ni kuhamasisha utalii wa ndani kwa Watumishi wa Serikali.



NA LUSUNGU HELELA-DODOMA

MKURUGENZI wa  Utawala na Raslimali Watu wa Wizara ya Maliasili na Utalii, Bw. Lusius Mwenda  ametoa wito kwa watumishi wa Serikali kuwa  mstari wa mbele  kutembelea vivutio vya utalii vilivyopo nchini kwa ajili ya kujifunza mambo mapya ikiwa  pamoja na kupumzisha akili.

Pia amewataka watumishi hao kujenga utamaduni wa kutembelea vivutio hivyo  ili waweze kuona na kuchangamkia  fursa mbalimbali za kiuchumi ambazo wanaweza kuanza kuzifanya kwa ajili ya kujiingizia kipato ikiwa ni  njia mojawapo ya kuanza kujiandaa kwa ajili ya kustaafu.

Amefafanua kuwa kila  mtumishi wa Serikali anatakiwa kuanza kujiandaa kwa ajili ya kustaafu kuanzia ile siku ya kwanza aliyoajiriwa.

Amesema watumishi walio wengi mara baada ya kustaafu hali zao za kiuchumi huteteleka  kwa vile katika kipindi cha utumishi wao walikuwa hawatembelei maeneo tofauti na yale  waliyoyazoea  kwa ajili ya kujifunza na kukutana na watu tofauti.

Ametoa Rai hiyo jana katika kituo cha utalii  Kolo kilichopo  wilayani Kondoa mkoani Dodoma   alipokuwa ameongozana na  Watumishi zaidi ya 50 kutoka Wizara ya Maliasili na Utalii , Ikiwa ni moja ya jitihada za Wizara hiyo kuhamasisha utalii wa ndani kwa Watumishi wa Serikali kwa kuanza na Watumishi wa Wizara yenye dhamana.

Kivutio cha Utalii, Kolo  kipo ni kivutio  mashuhuri sana kwa michoro yake ya miambani kwa vile inafanana na michoro ya Afrika Kusini na kimebeba tamaduni za waafrika.

" Tunataka Watumishi muwe mabalozi wazuri kuanzia kwenye ngazi ya familia hadi ngazi ya taifa kwa kuhamasisha jamii kuona umuhimu wa kutembelea vivutio vya utalii ikiwemo maeneo ya kihistoria  ambavyo yamesheheni chimbuko la tamaduni zetu pamoja na harakati za binadamu katika kupambana na mazingira yake." alisema

Akizungumzia kuhusu lengo la ziara hiyo, Bw.Mwenda amesema ziara hiyo ya siku moja imejikita kuhamasisha Utalii wa ndani kwa kauli mbiu " Utalii wa ndani unaanza kwako na kwangu" 

Aidha, Amesema Wizara ya Maliasili na Utalii inaandaa utaratibu maalum wa kuwawezesha watumishi wengine wa Wizara nyingine pamoja na taasisi za serikali waanze kutembelea vivutio vya utalii ili kujenga utamaduni kwa watumishi wa Umma kutembelea vivutio vya utalii nchini kwa ajili ya kujifunza na kufurahia maisha.



Awali, Mkuu wa Kituo cha Kolo, Zuberi Mabie alieleza kuwa Kolo ni kivutio cha Utalii cha aina yake chenye michoro ya miambani iliyochorwa na jamii ya Wasandawe miaka 10,000 hadi miaka 6,000 iliyopita.

Amesema eneo hilo ni miongoni mwa maeneo manne ya Idara ya Mambokale yaliyopo katika orodha ya Urithi wa dunia


Alisema inaonesha kuwa kabla ya ugunduzi huo watu walikuwa wanaweka kumbukumbu ya kuchora vitu na matukio waliyokuwa wanayaona katika mazingira yao.

Akizungumzia kuhusu idadi ya watalii wanaotembelea, alisema kila mwezi hupata watalii zaidi ya 200 kutoka ndani na nje ya nchi.

Kwa upande wake, Afisa Utalii, Heda Chale mara baada ya kutembelea kituo hicho alisema ameifurahia safari hiyo na amejifunza vitu mbalimbali ikiwa pamoja na kujionea madhari ya aina yake katika kivutio hicho.

Naye, Mhifadhi Mkuu wa Mambo Kale, Wiliam Mwita alitoa wito kwa jamii kutembelea vituo vya maeneo ya kihistoria  yaliyotapakaa nchi nzima ili jamii iweze kujifunza historia ya binadamu pamoja na mapambano yake katika kuyamudu mazingira.

Pia, Alitoa wito kwa Wawekezaji kuchangamkia fursa ya kuwekeza kwenye vivutio vya Mambokale kwa vile nafasi zipo wazi lengo likiwa ni kuviendeleza kwa ajili ya kizazi cha sasa na kijacho.

Amesema maeneo hayo yanahitaji uwekezaji wa nguvu ili kuyafanya yawe na mvuto ili kuwavutia wageni kutika nje na pia Watanzania

Kivutio cha Utalii Koli kipo kilomita 150 kutoka jiji la Dodoma na ni michoro ya kwanza kwa bara la Afrika kutokana na uwingi wake na kutapakaa kwake katika eneo kubwa.

No comments:

Post a Comment