HATUTAONGEZA MUDA WA UJENZI, NAIBU WAZIRI KWANDIKWA - THE HABARII

THE HABARII

HABARI | MATUKIO | MICHEZO.


ASAS GROUP

Habari Mpya


Saturday, 18 August 2018

HATUTAONGEZA MUDA WA UJENZI, NAIBU WAZIRI KWANDIKWA


Ujenzi wa daraja la Kikamba wilayani Songwe linalounganisha Mkoa wa Songwe na Katavi ukiendelea daraja hilo linatarajiwa kukamilika mwishoni mwa mwaka huu.


SERIKALI imesema haitamwongezea mkataba mkandarasi China Railway 15 Bureau Group Corporation anayejenga barabara ya Chunya –Makongolosi kwa kiwango cha lami muda wake utakapomalizika.

Naibu Waziri wa Ujenzi, Mhe. Elias John Kwandikwa amesema muda wa miezi 27 aliyopewa kujenga barabara hiyo yenye urefu wa KM 39 unatosha na hivyo ni jukumu lake kuhakikisha kuwa anakuwa na vifaa na wafanyakazi wa kutosha wakati wote.

“Mkishindwa kukamilisha barabara hii kwa wakati hamtapata tena kazi hapa nchini kwani mtakuwa mmeshindwa kazi kwa kukiuka mkataba na kuiongezea Serikali gharama”, amesema Mhe. Kwandikwa.

Naye Kaimu meneja wa wakala wa barabara (TANROADS) mkoa wa Mbeya Mhandisi Selemani Lawena amesema barabara ya Chunya –Makongolosi ni sehemu ya barabara ya Mbeya-Rungwa yenye urefu wa KM 293 ambayo inaunganisha kwa njia fupi mkoa wa Mbeya na mikoa ya Singida na Tabora.
“Barabara hii ikikamilika itafungua uchumi wa mikoa ya Mbeya na Songwe na kuhuisha shughuli za kilimo,mifugo, uchimbaji madini na ufugaji nyuki na hivyo kuongeza fursa za maendeleo kwa jamii na serikali kwa ujumla”, amesema mhandisi Lawena.
Mhandisi lawena amesema sehemu ya Mbeya- Chunya KM 72 imekamilika na ujenzi wa Chunya –Makongolosi KM 39 unatarajiwa kukamilika Januari 2020.
Katika hatua nyingine Naibu Waziri Kwandikwa amekagua ujenzi wa barabara ya mchepuo ya Iwambi-Mbalizi KM 6.5 jijini Mbeya  ambayo itatumiwa na magari madogo ili kupunguza msongamano na ajali katika mlima Mbalizi na kusisitiza umuhimu wa wadau wote wa usafiri kushirikiana ili kupunguza ajali na hivyo kulinda maisha na mali.
IMETOLEWA NA KITENGO CHA HABARI NA MAWASILIANO WIZARA YA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO

No comments:

Post a Comment