TAKUKURU YATOA ELIMU YA RUSHWA TANESCO SINGIDA, MENEJA ATOA MREJESHO WA KIKAO CHA NAIBU WAZIRI MKUU NA WAZIRI WA NISHATI - THE HABARII

ASAS GROUP

Habari Mpya


Monday 8 April 2024

TAKUKURU YATOA ELIMU YA RUSHWA TANESCO SINGIDA, MENEJA ATOA MREJESHO WA KIKAO CHA NAIBU WAZIRI MKUU NA WAZIRI WA NISHATI

Afisa wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) Mkoa wa Singida, Joseph Kailaga akitoa elimu Aprili 8, 2024 kwa watumishi wa Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) mkoani hapa iliyohusu madhara ya rushwa mahala pa kazi na athari zake.

Na Mwandishi Wetu, Singida

WATUMISHI wa Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) Mkoa wa Singida wametakiwa kuteleza majukumu yao kwa kufuata misingi ya sheria, kanuni, taratibu na miongozo iliyopo ili kujiepusha na vitendo vya rushwa.

Afisa wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) Mkoa wa Singida, Joseph Kailaga aliyasema hayo Aprili 8, 2024 wakati akitoa elimu kwa watumishi hao iliyohusu madhara ya rushwa mahala pa kazi na athari za kuomba na kupokea rushwa.

Kailaga alisema pia TAKUKURU wameweza kuwakumbusha wafanyakazi hao wanapotekeleza majukumu yao wafuate miongozo na sheria ili kujiepusha na vitendo vyovyote vya rushwa na kuwa athari ya vitendo hivyo ni kubwa sana katika jamii.

"Tumewataka watumishi hao wanapokuwa wakiwaungania wananchi umeme wafuate taratibu na miongozo waliojiwekea katika kutekeleza majukumu yao bila ya kujihusisha na vitendo vya rushwa, " alisema Kailaga.

Kailaga alisema TAKUKURU inawashukuru Tanesco kwa kufanya maboresho ya  wateja wao kutumia mfumo wa kuomba maombi yao ya kuingiziwa umeme  kwa njia ya kielekritoniki ambayo imepunguza urasimu na vitendo vya rushwa kwa kuonana na mtu mmoja mmoja ofisini na baada ya kujaza fomu ya maombi ataenda kufanyiwa taratibu za kupimiwa na kuandikiwa michoro katika nyumba yake na kuwekewa umeme.

Aidha, Kailaga alisema Serikali imeweka utaratibu huo ambao umepunguza vitendo vya rushwa kwa watumishi wa Tanesco kwa kutumia mfumo huo na wao kama TAKUKURU wamepongeza utaratibu huo.

Alisema watumishi hao wa Tanesco baada ya kupata elimu hiyo wameahidi kuwa mabalozi wazuri kwa kutoshiriki vitendo vya rushwa na kuwa watatekeleza majukumu yao kwa weledi na kufuata maadili ili kutokomeza vitendo vya rushwa.

Meneja wa Tanesco Mkoa wa Singida Mhandisi Mwamvita Ally akitoa mresho kwa watumishi hao  kutoka kwa Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Doto Biteko baada ya kufanyika kikao hivi karibuni jijini Mwanza aliwapongeza watumishi hao kwa uvumilivu wao katika kipindi kigumu walichopitia cha mgao wa umeme ambapo waliweza kuwahudumia wateja wao vizuri licha ya kuwepo kwa malalamiko mengi lakini walipambana hadi hali ya upatikanaji wa umeme ilipokuwa nzuri.

Mhandisi huyo alisema mambo mengine aliyoyagiza kwa watumishi hao ni jinsi shirika hilo lilivyokuwa limechafuka kwa vitendo vya rushwa ambapo aliwata kutoka kwenye uchafu huo na kulisafisha ili jamii iwe na imani nalo kwa kufanya kazi kwa kufuata maadili na kufuata sheria za utumishi wa umma na kutoa lugha nzuri wanapowahudumia wateja wao.

Asiatu Mnanura akizungumza kwa niaba ya watumishi wa shirika hilo aliwashukuru TAKUKURU na TANESCO kwa kuwapa elimu hiyo ambayo imewaongezea uwezo mbalimbali wa kujiepusha na vitendo vya rushwa na kuwa wataendelea kukumbusha kuhusu jambo hilo na kuwa mabalozi wazuri wa kupinga rushwa.

Afisa wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) Mkoa wa Singida, Joseph Kailaga akisisitiza jambo wakati akitoa elimu hiyo.
Meneja wa Tanesco Mkoa wa Singida, Mhandisi Mwamvita Ally akitoa mrejesho kwa watumishi wa shirika hilo kutoka kwa  Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati Dkt. Doto Biteko. 
Afisa Utumishi na Rasilimali Watu (HR) wa Shirika hilo Mkoa wa Singida, Deogratius Jackson akizungumza wakati wa utoaji wa elimu hiyo.
Mtumishi wa Tanesco, Manase Mkuki akichangia jambo wakati wa utoaji wa elimu hiyo.
Asiatu Mnanura akizungumza kwa niaba ya watumishi wenzake waliopata elimu hiyo.
Charles Mkojera akichangia jambo kwenye mafunzo hayo.
Bakari Msacky akichangia jambo.
Watumishi wa Tanesco Mkoa wa Singida wakipata elimu hiyo ya rushwa.
Elimu hiyo ikiendelea kutolewa.

Watumishi wa Tanesco Mkoa wa Singida wakipata elimu hiyo ya kukabiliana na vitendo kazini

 Taswira ya utoaji wa elimu hiyo.

No comments:

Post a Comment