CHUO CHA MALYA NI FURSA KWA TAIFA - THE HABARII

ASAS GROUP

Habari Mpya


Sunday 4 June 2023

CHUO CHA MALYA NI FURSA KWA TAIFA

Katibu Mkuu Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo Bw. Saidi Yakubu (wa pili kushoto) akitembelea mradi wa ujenzi wa hosteli ya wanachuo inayojengwa Chuo cha Maendeleo ya Michezo Malya Juni 02, 2023 wakati wa ziara yake ya kikazi chuoni hapo kukagua miradi ya maendeleo inayotekelezwa na chuo hicho.

Katibu Mkuu Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo Bw. Saidi Yakubu akimwagilia maji mti alioupanda Chuo cha Maendeleo ya Michezo Malya Juni 02, 2023 wakati wa ziara yake ya kikazi chuoni hapo kukagua miradi ya maendeleo inayotekelezwa na chuo hicho.

Na Eleuteri Mangi, WUSM, Mwanza

KATIBU Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo Bw. Saidi Yakubu amesema Chuo cha Maendeleo ya Michezo Malya ambacho kipo chini ya wizara hiyo kina fursa lukuki kwa taifa na kwa wahitimu wake kwenye soko la ajira nchini.

Bw. Yakubu amesema hayo Juni 02, 2023 wakati wa ziara yake ya kikazi chuoni hapo kukagua miradi ya maendeleo ya chuo hicho kilichopo wilaya ya Kwimba mkoani Mwanza, na ameahidi kuwa, Wizara itatoa mipira 100 ambayo itatumiwa kujifunzia na kufundishia ili kuandaa wataalam wa michezo waliobobea katika michezo nchini.

"Chuo cha Maendeleo ya Michezo Malya, ni chuo cha kipekee katika ukanda wa Afrika Mashariki na Kati, ni lazima tukienzi, hii ni tunu kwa taifa kwa kutoa wataalam wa michezo. Tofauti na vyuo vingine, hapa asilimia 95 ya wanachuo tayari wana ajira ambazo ni chache sana katika mahitaji mengi” amesema Bw. Yakubu.

Takwimu za Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia zinaonesha zipo shule za msingi 19,000 na sekondari 4000, ikiwa kila shule ikipata mwalimu mmoja wa michezo maana yake kuna mahitaji ya walimu wa michezo 21,000 kati ya walimu 23,000 wanaohitajika hapa nchini.

Kwa mantiki hiyo, wataalam wa michezo wanaozalishwa na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam ni 704 wakati Chuo cha Malya kimezalisha wataalam wa michezo 701 na kufanya idadi ya wataalam wa michezo nchini kuwa chini ya 2000 nchi nzima. 

Naye Mkuu wa Chuo hicho Bw. Richard Mganga, amesema kuwa Chuo hicho kina uwezo wa kudahili wanachuo 400 katika ngazi ya Astashahada na Diploma ya michezo katika fani Elimu ya Viungo na Michezo, Usimamizi wa na Utawala katika Michezo pamoja na Elimu ya Ukufunzi wa Michezo.

Kwa upande wake rais wa Serikali ya wanafunzi Baptista Kapinga amesema kuwa ipo mstari wa mbele kuongeza nguvu katika michezo, hivyo ni wakati wa wataalam wa michezo kutumia taaluma yao na kuifanya michezo kuendeshwa kibiashara na kuinua maisha ya watu na jamii kwa ujumla.


No comments:

Post a Comment