DC MWENDA AZINDUA ZAHANATI YA KIJIJI CHA MASAGI ILIYOJENGWA KWA MIL.99/- - THE HABARII

ASAS GROUP

Habari Mpya


Friday 12 May 2023

DC MWENDA AZINDUA ZAHANATI YA KIJIJI CHA MASAGI ILIYOJENGWA KWA MIL.99/-

Mkuu wa Wilaya ya Iramba, Suleiman Mwenda akikoroga uji wa Lishe ulikuwa unagawiwa kwa Watoto waliofika kwenye uzinduzi wa Zahanati ya Kijiji cha Masagi iliyopo Kata ya Mtoa Tarafa ya Shelui wilayani hapa iliyojenga kwa zaidi ya Sh.Milioni 99 katika hafla iliyofanyika juzi.

Na Mwandishi Wetu, Iramba

MKUU wa Wilaya ya Iramba Mkoani Singida, Suleimani Yusuph Mwenda,  amezindua rasmi Zahanati ya Kijiji cha Masagi Kata ya Mtoa Tarafa ya Shelui wilayani hapa iliyojenga kwa zaidi ya Sh.Milioni 99 ambayo  itahudumia wananchi  3,117 wa  kijiji hicho..

 Akizungumza baada ya kuzindua zahanati hiyo,  Mwenda, amewataka wananchi hao kuhudhuria kikamilifu na kupata matibabu katika zahanati hiyo kwani kwa sasa changamoto ya kufuata matibabu kwa mwendo mrefu umeisha.

Alisema  kuzinduliwa kwa Zahanati hiyo kutaondoa  kabisa vifo vya akina Mama na watoto  ambao walikuwa wakitembea umbali mrefu kufuata  matibabu Shelui au Mtoa  na katika Hospitali ya Wilaya.

"Vifo vya akina mama vitapungua kwa asilimia kubwa  kutokana na kukamilika kwa Zahanati nyingi katika vijiji Wilayani Iramba, lakini pia pindi vituo vya Afya vya Mtoa, na Shelui vitakapokamilika vitafanya vifo vya mama na mtoto kuwa ni historia katika wilaya yetu," alisema.                            

Aliongeza kuwa Sh. Milioni 280 zimeletwa kumalizia ujenzi wa Kituo cha Afya Mtoa, ambapo Sh. Milioni 120 zimeingia tayari kwa ajili ya Kukamilisha Kituo Cha Afya Shelui na Sh.Milioni ni 200 zimeletwa Kukamilisha ujenzi wa  Zahanati ya Kinambeu  lengo kusogeza huduma za matibabu karibu kwa wananchi..

Naye Mganga Mkuu wa Wilaya ya Iramba Dkt. Hussein Sepoko, alisema  Zahanati ya Masagi  imekamilika na tayari imepewa  vifaa tiba vyenye thamani ya Sh.  Milioni 24 huku wahudumu wa afya wawili tayari wamefika  kwa ajili ya kuwahudumia wananchi.

Aidha, wananchi wa Kijiji hicho wameishukuru serikali ya awamu ya Sita inayoongozwa na Rais Dk. Samia Suluhu Hassan kwa kuwajali na kuwajengea zahanati karibu ambayo itawafanya sasa wasitembee umbali mrefu kufuata huduma za matibabu.

Mkuu wa Wilaya ya Iramba, Suleiman Mwenda, akizungumza na wananchi (hawapo pichani) wakati wa hafla ya uzinduzi wa zahanati hiyo.

Mkuu wa Wilaya ya Iramba, Suleiman Mwenda akipata maelezokutoka kwa mmoja wa wazee wakati wa hafla hiyo.

Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Iramba Mhe. Innocent Msengi akizungumza katika hafla hiyo.

Mganga Mkuu wa Halmashauri ya Wilaya ya Iramba Dr. Hussein Sepoko akisoma taarifa ya Utekelezaji wa Mradi wa Zahanati ya Masagi.

UjiLishe ukiandaliwa.
Mkuu wa Wilaya ya Iramba, Suleiman Mwenda akigawa uji lishe kwa wananchi waliokuwepo kwenye uzinduzi huo.
DC Mwenda akiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya viongozi wa wilaya hiyo.

Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Iramba Mhe. Innocent Msengi akigawa uji wa lishe  kwa wananchi waliokuwepo kwenye uzinduzi huo. 

No comments:

Post a Comment