BARABARA YA MAKETE-MBEYA KUFUNGUKA KWA LAMI - THE HABARII

ASAS GROUP

Habari Mpya


Thursday 29 December 2022

BARABARA YA MAKETE-MBEYA KUFUNGUKA KWA LAMI

Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, Prof. Makame Mbarawa akisisitiza jambo kwa wananchi wa Wilaya ya Makete, Mkoani Njombe, kabla ya hafla ya utiaji saini Mkataba wa ujenzi wa barabara ya Kitulo hadi Iniho KM 36.3 kwa kiwango cha Lami Wilayani Makete.

Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Barabara Nchini (TANROADS) Mhandisi Rogatus Mativila akiwa na Muwakilishi wa Kampuni ya M/S China National Aero-Technology Engineering Corporation (wa pili kulia) wakionyesha mkataba wa Ujenzi wa Barabara  ya Kitulo hadi Iniho KM 36.3 kwa kiwango cha Lami, mara baada ya kuusaini Wilayani Makete, Mkoani Njombe.

WAZIRI wa Ujenzi na Uchukuzi, Prof. Makame Mbarawa amesema Serikali itaendelea na ujenzi wa barabara za lami  katika mikoa ya nyanda za juu kusini ili kuunganisha vema ukanda huo na bandari ya Mtwara na hivyo kurahisisha shughuli za usafiri na usafirishaji, kukuza uzalishaji wa mazao ya kilimo, misitu na kukuza utalii.

Akizungumza katika hafla ya utiaji saini ujenzi wa barabara ya Isyonje-Kikondo hadi Makete KM 96.2 sehemu ya Kitulo hadi Iniho KM 36.3 inayojengwa kwa kiwango cha lami Waziri Prof. Mbarawa amesema Serikali ya awamu ya sita itahakikisha inaunganisha kwa njia fupi mikoa ya Mtwara, Ruvuma, Njombe hadi Mbeya kupitia Makete ili kukuza fursa za kiuchumi zilizoko katika ushoroba huo.


“Serikali inayoongozwa na Rais Dkt. Samia imejikita kwenye kuboresha miundombinu hususani maeneo yenye uzalishaji mkubwa hivyo niwahakikishie kuwa ongezeni uzalishaji miundombinu bora inakuja,’ amesisitiza Waziri Prof. Mbarawa.


Ameitaka Wakala wa Barabara nchini (TANROADS), kumsimamia kikamilifu Mkandarasi anayejenga barabara hiyo M/S China National Aero-Technology Egineering Corporation ili mradi huo ukamilike kwa wakati na viwango.


Mtendaji mkuu wa TANROADS Mhandisi Rogatus Mativila  amesema ujenzi wa barabara hiyo utahusisha ujenzi wa mizani katika Kijiji cha Igalala ili kudhibiti magari yanayozidisha uzito hivyo kuwataka wananchi kuzingatia sheria na kulinda miundombinu yote ya barabara. 


Kwa upande wake Mbunge wa Makete Festo Sanga ameishukuru Serikali kwa kutoa fedha kwa ajili ya mradi huo kwani kukamilika kwake kutaunganisha wilaya hiyo na Mkoa wa Mbeya kwa njia fupi, kukuza utalii wa hifadhi ya taifa Kitulo na kupandisha thamani ya mazao mbalimbali yanayozalishwa Mkoani Njombe.


Mkuu wa mkoa wa Njombe Bw, Anthon Mtaka amewataka wakazi wa wilaya ya Makete kote nchini kutumia maendeleo ya ujenzi wa miundombinu kuwekeza wilayani humo.


Zaidi ya shilingi bilioni 69.7 zinatarajiwa kutumika katika ujenzi huo unaotarajiwa kutekelezwa katika kipindi cha miezi 36.


No comments:

Post a Comment