NAFASI YA KUCHAGUA AIDHA KUWA NG'OMBE AU NGURUWE - THE HABARII

ASAS GROUP

Habari Mpya


Tuesday 23 November 2021

NAFASI YA KUCHAGUA AIDHA KUWA NG'OMBE AU NGURUWE


Na Adeladius Makwega, Mbagala

JUMAPILI ya Novemba 21, 2021 nilishiriki ibada ya uzinduzi wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania Dayosisi ya Dodoma Usharika wa Chamwino Ikulu Mtaa wa Nazareth Buigiri. Ibada hiyo ya uzinduzi wa kanisa hili iliongozwa na Baba Askofu Amon Kinyunyu ambaye ndiye Mkuu wa Kanisa hilo kwa Dayosisi ya Dodoma.

Baba Askofu Kinyunyu wakati wa utangulizi wa mahubiri yake katika ibada hiyo alitolea mtano suala la mtu anayekula nyama ya Ng’ombe na yule alaye nyama ya Nguruwe. Kulingana na imani ya Kikristu zote hizo ni nyama halali, Je Baba Askofu Kinyunyu alisema nini? 

Baba Askofu Kinyunyu akitolea mfano huu kwa mtu anayekula nyama ya ng’ombe kwanza kabisa mtu husika uandaa mnyama huyu na kumchinja, akishachinjwa mnyama huyo ngozi ya ng’ombe inatenganishwa na mnyama alafu nyama yake hukatwa vipande vipande kuchukuliwa na mpishi kwa ajili ya kupikwa na kuliwa.

Mara baada ya nyama kutenganishwa, ngozi ya ng’ombe huanikwa vizuri sana kwa ajili ya matumizi mengine iwe kama kuwambia ngoma, kutengenezea viatu, mikoba na mikanda na kadhalika.

Kwa yule anayetaka kula nyama ya nguruwe anapaswa kumchukua mnyama huyo na kumchinja alafu kuikatakata nyama hiyo katika vipande na yule mpikaji huichukua na kuipika na kuwa tayari kuliwa.

Baba Askofu Kinyunyu anasema kuwa ngozi ya nguruwe huwa inaliwa pamoja na nyama. Kwa hiyo nyumba aliyochijwa nguruwe ni vigumu kukuta ushahidi wowote ule lakini nyumba iliyochinjwa ng’ombe ndugu yangu ushahidi unapatikana.

Unaweza Kusema,

“Jamani mbona naona ngozi na mie naombeni kipande cha nyama.”

Baba Askofu Kinyunyu alifananisha wanyama hao wawili na maisha ya binadamu yalivyo kila mmoja wetu popote alipo iwe shambani, kwenye uvuvi kwenye ufugaji au katika nafasi ya uongozi unaweza kuchangua kuwa kama mnyama gani kati ya hao wawili.

Uamuzi wakuchagua kuwa ng’ombe au nguruwe upo katika matendo ya yule anayetenda maana baada ya hapo ushahidi utaonekana iwe kuacha ngozi au kutoacha kitu.

Baba Askofu Kinyunye alitolea mfano huo akiwapongeza wanausharika wa Chamwino Ikulu, Mtaa wa Nazareth Buigiri kwa wale waliofanikisha ujenzi wa Kanisa la Usharika huo ambapo alisema kuwa hata kama hawatakuwepo dunia ujenzi wa jengo hili utakuwa sawa na yule aliyechinja ng’ombe na kuila nyama yote lakini ngozi imesali na kila mmoja wetu anaiona.

Kwa hiyo kila mmoja wetu anayo nafasi ya kuchagua mnyama wake iwe nguruwe au ng’ombe, Je wewe ni nani? Msomaji wa matini hii nakupa muda wa kutafakari hapo ulipo au popote ulipo angalia jamii yako alafu mchagulie anayekuongoza kati ya wanyama hao wawili. Kumbuka kufanya kwa siri, moyoni mwako. Nina hakika umetafakari, umepata jibu kama ni NG’OMBE /NGURUWE kumbuka jibu lako liwe la haki bila upendeleo wowote NG’OMBE /NGURUWE.

Basi kwa leo naishia hapo, nakutakia siku njema.

makwadeladius@gmail.com

0717649257 


No comments:

Post a Comment