Fukwe ya Mhalo ziwa Nyasa unaweza kuona mipaka ya nchi mbili kwa wakati mmoja.
Watalii wa ndani
wakiwa katika fukwe ya Mhalo Mbambabay ziwa Nyasa.
Mhalo Beach Lodge
ambayo imejengwa ufukweni inayotoa huduma mbalimbali za chakula na malazi kwa
wageni.
WILAYA ya Nyasa mkoani Ruvuma imebarikiwa kuwa na fukwe za asili katika ziwa Nyasa ambazo hazifanani na fukwe nyingine zozote duniani na endapo zitaendelezwa zinaweza kuwa chanzo muhimu cha mapato kwa serikali na wananchi.
Fukwe ya Mhalo
iliyopo katika kijiji cha Ruhekei Kata ya Kilosa Halmashauri ya Wilaya ya Nyasa
imeendelezwa kwa kujengwa vivutio vya utalii pamoja na hoteli ya Mhalo beach
Lodge iliyojengwa mwambao mwa fukwe za Mhalo.
Benado Lisambo ni
Meneja wa Mhalo Beach Lodge anasema fukwe hizo zina maajabu ambayo hayawezi
kupatikana sehemu nyingine hali ambayo inavutia wageni wengi wa ndani na nje ya
nchi kufanya utalii na kupata huduma zote zinazostahili kwa watalii.
Anakitaja kivutio
kikubwa katika fukwe hizo kuwa ni mtalii anaweza kuona mipaka miwili ya nchi
mbili za Malawi na Msumbiji kwa wakati mmoja jambo ambalo linawavutia watalii
wengi wanaotembelea fukwe hizo.
“Sisi wilaya Nyasa
tuna bahati sana, ukiwa hapa Mhalo beach ukiangalia kusini unaona milima ya
nchi ya Msumbiji na ukiangalia Magharibi unaona milima ya nchi ya Malawi, wakati
wa usiku unaweza kuona taa za magari katika nchi hizo kwa kweli inavutia sana,’’
anasisitiza Lisambo.
Hata hivyo anasema
fukwe yote ya Mhalo inavutia wageni wengi wa ndani na nje ya nchi kwa sababu
haina uchafu, maji yake ni maangavu hali ambayo inamwezesha mtalii kuwaona
samaki wanavyotembea ndani ya maji
katika ziwa Nyasa.
Kulingana na Meneja
huyo, toka fukwe ya Mhalo hadi mpakani na nchi ya Msumbiji ni umbali wa
kilometa 30 na kwamba unaweza kusafiri kwa boti kupitia ziwa Nyasa na kwamba kusafiri kwa boti toka fukwe ya Mhalo hadi
nchini Malawi ni safari ya saa sita.
Anawataja watalii
ambao wametembelea fukwe za Mhalo kuwa wametoka nchi za Ujerumani, Italia, Uingereza, Marekani, Japan,
Afrika ya Kusini, Malawi, Msumbiji, Zimbabwe na kwamba wanapokea pia watalii
wengi kutoka ndani ya nchi.
“Watalii wakifika
hapa Mhalo beach kuna vivutio vingi, wanaweza kufanya utalii wa kuogelea, kupanda
milima ya Livingstone, kutembea ufukweni kilometa mbili, kuona ngoma za asili
mwambao mwa ziwa Nyasa, ikiwemo ngoma ya mganda, kioda na lindeku na kufanya
safari za majini kwa kutumia boti’’, anasema Lisambo.
Joseph Ndomondo
Mwongoza watalii Mkazi wa Liuli ziwa Nyasa anasema fukwe za ziwa Nyasa upande
wa Tanzania ni bora zaidi kwa kuwa ni za asili ambazo zimetengenezwa na
Mwenyezi Mungu mwenyewe.
“Fukwe za ziwa Nyasa
upande wa Malawi zimetengenezwa toka kingo za milima hivyo zimechimbwa hali
ambayo inadhihirisha ubora wake hauwezi kulingana na fukwe za ziwa Nyasa upande
wa Tanzania’’, anasema Ndomondo.
Afisa Maliasili na
Utalii wa Halmashauri ya Wilaya ya Nyasa Bugingo Bugingo anasema ziwa hilo
limebarikiwa kuwa na fukwe nzuri za asili na zinazofaa kwa uwekezaji kwenye
sekta ya utalii hivyo ametoa rai kwa wawekezaji kuwekeza ziwa Nyasa.
Imeandikwa na Albano Midelo
Afisa Habari Mkoa wa Ruvuma.
No comments:
Post a Comment