DKT.ABBASI KUENDELEA KUWA MSEMAJI WA SERIKALI - THE HABARII

ASAS GROUP

Habari Mpya


Monday 3 February 2020

DKT.ABBASI KUENDELEA KUWA MSEMAJI WA SERIKALI

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt John Pombe Magufuli
akimuapisha Dkt. Hassan Abbasi kuwa Katibu Mkuu Wizara ya Habari,
Utamaduni, Sanaa na Michezo katika  hafla iliyofanyika Ikulu jijini
Dar es salaam Februari 3, 2020.

Na Anitha Jonas – WHUSM
RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania  Dkt.John Pombe Magufuli amesema kuwa Katibu Mkuu wa  Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Dkt.Hassan Abbasi Said ataendelea kuwa Msemaji Mkuu wa Serikali .
Dkt.Magufuli ameyasema hayo leo Ikulu jijini Dar es Salaam katika hafla ya kuwaapisha viongozi mbalimbali aliyowateua hivi karibuni.
Katika hafla hiyo Rais Magufuli alisisitiza kuwa kabla ya uteuzi huo Dkt.Abbasi alipokuwa Mkurugenzi wa Idara ya Habari Maelezo na Msemaji Mkuu wa Serikali alifanya kazi nzuri ya kuisemea serikali kwa kushirikiana na Waziri wa wizara hiyo Dkt.Harrison Mwakyembe na menejimenti.
“Ningependa aendelee kuwa msemaji wa Serikali lakini mahali mtu anapotakiwa kupata promosheni kwa sababu ni Motivating Agent ndiyo maana  nimemteuwa kuwa Katibu wa Wizara hiyo na kwa sasa hivi ataendelea kuwa Msemaji wa Serikali mpaka tutakapo pata mwingine”alisema Mhe.Rais Magufuli.
Katika kipindi cha uongozi wake alitangaza miradi ya Serikali, pamoja na kueleza utekelezaji wa mikakati mbalimbali inayoendelea kufanyika pamoja na kuanzisha kipindi cha viongozi kusema  utekelezaji wa majukumu ya taasisi zao kupitia Kipindi cha TUNATEKELEZA kinachorushwa hewani na Televisheni ya TBC 1 katika mwaka mpya wa 2020 alianzisha kauli mbiu ya TUMEAMUATUNATEKELEZA2020.
Aidha Viongozi wengine walioapishwa katika hafla hiyo ni Makatibu Wakuu 05,  Makatibu Tawala wa mikoa 03, Kamishina Jenerali wa Magereza na Kamishna Jenerali wa zimamoto na uokoaji, Kamishina wa ardhi Wizara ya Ardhi,Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Msajili wa Mahakama ya Rufani, Msajili wa Mahakama Kuu na wajumbe 03 wa Tume ya Utumishi wa Mahakama.

No comments:

Post a Comment