RC MAKONDA: CHANGAMKIENI FURSA YA KUTIBIWA MOYO - THE HABARII

ASAS GROUP

Habari Mpya


Wednesday 26 June 2024

RC MAKONDA: CHANGAMKIENI FURSA YA KUTIBIWA MOYO

WANANCHI wa Mkoa wa Arusha na mikoa ya jirani wametakiwa kuchangamkia fursa ya kupima magonjwa mbalimbali yakiwemo ya moyo huduma inayotolewa bila malipo yoyote yale katika kambi ya matibabu ya siku saba inayofanyika katika uwanja wa Sheikh Amri Abeid.

Rai hiyo imetolewa leo na Mkuu wa mkoa huo Mhe. Paul Makonda wakati akizungumza na wananchi waliokuwa wanasubiri kupata huduma za kibingwa za uchunguzi na matibabu ya moyo zinazotolewa katika banda la Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI).

Mhe. Makonda alisema wataalamu kutoka JKCI wakiongozwa na Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi hiyo Dkt.Peter Kisenge wako katika uwanja huo kwaajili ya kutoa huduma za ushauri, upimaji na matibabu ya magonjwa ya moyo.

“Dkt. Kisenge ni daktari bingwa wa magonjwa ya moyo na mishipa ya damu, kumpata daktari huyu ambaye pia ni Mkurugenzi Mtendaji siyo jambo rahisi leo hii yupo hapa kwetu amekuja kutuhudumia wananchi tuitumie nafasi hii vizuri kwa kuja kupima afya za mioyo yetu”, alisema Mhe. Makonda.

Kwa upande wake Dkt. Kisenge alisema tangu waanze upimaji huo siku ya jana hadi leo wameona zaidi ya wagonjwa 200 na asilimia 45 ya waliowaona walikuwa na tatizo la shinikizo la juu la damu na kuna ambao wameshaanza kupata madhara ya ugonjwa huo.

“Tumewapa rufaa wagonjwa 30 hadi sasa ambao watakwenda kutibiwa katika taasisi yetu kati yao 18 tutawachunguza mishipa ya damu ya moyo ambayo inaonekana imeziba na kushindwa kupitisha damu vizuri. Wengine wanamatatizo ya mfumo wa umeme wa moyo na mioyo yao kufanya kazi katika kiwango cha chini”, alisema Dkt. Kisenge.

Mkurugenzi huyo mtendaji alisema katika kambi hiyo wanawashirikiana na wataalamu kutoka hospitali mbalimbali za Arusha ambao wanawajengea uwezo wa jinsi ya kuwatibu na kuwatambua wagonjwa wa moyo.

Kwa upande wa wananchi waliopata huduma ya matibabu katika banda la Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) walishukuru kwa huduma waliyoipata na kusema kuwa imewasaidia kujua hali za afya za mioyo yao.

Francis Noor mkazi wa Arusha aliwaomba wakuu wa mikoa mingine kuiga mfano wa mkuu wa mkoa wa Arusha Mhe. Paul Mkonda ili wafanye kambi za uchunguzi na  matibabu ya magonjwa mbalimbali ambazo zitawasaidia wananchi wenye vipato vya chini kupata huduma za kibingwa za matibabu.

“Nimefika hapa katika banda la Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete nimepata huduma za matibabu ya moyo na vipimo ambavyo sikutegemea kuvipata nimeonana na Dkt. Kisenge amenihudumia vizuri na kunipa ushauri”.

“Ninamshukuru Mwenyezi Mungu kupitia Rais wetu Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan na mkuu wa mkoa Mhe. Makonda ambao wamefanikisha kupatikana kwa huduma hii , mimi unavyoniona unaweza kusema nina hela nyingi lakini uchumi wangu ni wa hali ya chini. Miaka minne iliyopita niliandikiwa kufanya vipimo vya moyo nikashindwa kutokana na hali ya uchumi lakini leo hii nimeweza kupata huduma hii”, alishukuru Noor.

 “Ninashukuru kwa huduma niliyoipata ninawaomba wananchi wenzangu waje kupata huduma ya uchunguzi na matibabu ya moyo ambayo inatolewa bila malipo yoyote yale. Ninawashukuru viongozi wetu kwa kutujali sisi wananchi wanyonge wenye kipato cha chini”, alishukuru Etropia Nikolaus.

No comments:

Post a Comment