WAZIRI MAKAMBA ATETA NA WATUMISHI WA WIZARA - THE HABARII

THE HABARII

HABARI | MATUKIO | MICHEZO.


ASAS GROUP

Habari Mpya


Thursday, 14 December 2023

WAZIRI MAKAMBA ATETA NA WATUMISHI WA WIZARA

 Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. January Makamba (Mb) amekutana na kuzungumza na watumishi wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki jijini Dodoma.

 

Akizingumza katika kikao na wafanyakazi hao, Waziri Makamba amewataka watumishi wa Wizara kuendelea kufanya kazi kwa bidii na kuzingatia weledi ili kuleta matokeo yanayotarajiwa na hivyo kuiletea nchi maendeleo 

 

Waziri Makamba pia amewataka watumishi wa Wizara kuhakikisha mienendo na matendo yao viakisi Wizara wanayoifanyia kazi.

 

Amesema Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki inaakisi muonekano wa nchi mbele ya mataifa mengine.

 

“Wizara inatazamwa kama taswira ya nchi, ni muhimu kuhakikisha mnazingatia namna mnavyoishi, mnavyovaa na mnavyoongea pia, kiujumla ni mwenendo na muonekano wenu ndivyo ambavyo nchi inavyoonekana au kuchukuliwa, nyinyi ni kioo cha nchi” alisisitiza Mhe. Waziri Makamba.

 

Amesema Wizara imepanga kuboresha mazingira ya kazi na kujenga udugu, urafiki ili kumfanya kila mtumishi kuipenda kazi yake.

 

Amesema uamuzi huo unatokana na ukweli kuwa mtumishi anatumia muda mwingi ofisini kuliko sehemu nyingine hivyo kuboresha mazingira husika ni jambo la msingi

 

Akiongelea changamoto mbalimbali zinazoikabili Wizara Waziri Makamba ameahidi kuzifanyia kazi ili kutimiza nia yake ya kuwa na mahala bora pa kufanyia kazi na hivyo kutoa matokeo yanayotarajiwa.

 

Kikao hicho kimehudhuriwa na Naibu Waziri Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe. Balozi Mbarouk Nassor Mbarouk (Mb), Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Balozi Dkt. Samwel Shelukindo, Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki anayeshughulikia Afrika Mashariki Balozi Stephen Mbundi, Wakurugenzi, watumishi wa Wizara na Wakuu wa Taasisi zilizo chini ya Wizara.

No comments:

Post a Comment