![]() |
| Wawakilishi wa Asasi za Kiraia zinazojihusisha na maswala ya elimu wakichangia wakati wa mazungumzo hayo katika ofisi za CAMFED jijini Dar es Salaam. |
MWENYEKITI wa Bodi ya Wakurugenzi wa Taasisi ya Ushirikiano wa Elimu Duniani (GPE), Mheshimiwa Dr. Jakaya Mrisho Kikwete, Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, pamoja na Afisa Mtendaji Mkuu wa GPE, Bibi Laura Frigenti, wamekutana na kuzungumza na wawakilishi wa Asasi za Kiraia zinazojihusisha na maswala ya elimu katika ofisi za Taasisi ya Campaign for Female Education (CAMFED) tawi la Tanzania jijini Dar es Salaam leo.
Mkurugenzi wa CAMFED Tanzania, Bibi Nasikiwa Duke, ameeleza kuwa lengo kuu la mazungumzo hayo ilikuwa ni kutoa msisitizo wa umuhimu wa kuipa kipaumbele sekta ya elimu katika ajenda za kijamii na kisiasa.
Akiuongea baada ya kikao hicho Bi. Duke alisema mazungumzo hayo yalizingatia pia majukumu muhimu ya Asasi za Kiraia katika kusaidia juhudi za serikali kuboresha sekta ya elimu na kuchangia kikamilifu kwenye mijadala ya kisera katika makundi ya elimu ya ndani na wadau wa sekta hiyo.
"Mazungumzo hayo yalitoa fursa kwa wawakilishi wa Asasi hizo za Kiraia kushirikiana na kubadilishana uzoefu wao Pamoja na mafanikio yo katika kusaidia maendeleo na mabadiliko ya mfumo wa elimu.
Kikao hicho kiliwaleta pamoja wadau muhimu ili kuzungumzia umuhimu wa juhudi za pamoja kuisaidia juhudi za serikali katika kukuza elimu, haswa katika mikoa inayokabiliana na mahitaji makubwa zaidi," Bi Duke alifafanua.
GPE ni mfuko mkubwa zaidi wa duniani uliojitolea kusaidia maswala ya maendeleo ya utoaji wa elimu bora katika nchi zenye kipato cha chini na kuhakikisha kwamba kila mtoto, bila kujali jinsia, anapata fursa, matumaini na uwezo wa kusoma.
Katika miongo miwili iliyopita, GPE imekuwa ikitoa fedha na misaada kukuza mfumo wa elimu imara na thabiti katika nchi zilizoathiriwa na umaskini mkubwa au migogoro ili kuwezesha watoto wengi zaidi, haswa wasichana, kupata elimu inayohitajika kwa ukuaji binafsi na kuchangia kujenga ulimwengu wenye ustawi endelevu.
Kwa upande mwingine, CAMFED ni Taasisi iiliyojizatiti kushughulikia utoaji elimu kwa wasichana, kupitia mfumo wa uwajibikaji wa vijana na jamii unaoshajihisha matarajio ya wasichana kuwa wanawake huru na wenye ushawishi.
CAMFED inaendeshwa na kamati na timu za mitaa zinazojumuisha wahitimu, walimu, wazazi, maafisa wa serikali, na wadau wengine wa kujitolea ambao hutenga muda na kutumia utaalam wao kuhakikisha kuwa wasichana wengi wanamaliza elimu yao kwa mafanikio.
.jpg)



No comments:
Post a Comment