| Muonekano wa kichwa cha treni (locomotive) kilichokarabatiwa katika Karakana Kuu ya TAZARA jijini Dar es Salaam. |
NAIBU Waziri wa Ujenzi
na Uchukuzi, Eng. Godfrey Kasekenya ameitaka Menejimenti ya Mamlaka ya Reli
Tanzania na Zambia (TAZARA), kubuni mikakati ya kibiashara inayoweza
kutekelezeka na kupimika ili kuliwezesha shirika hilo kutoa huduma bora na
kupata faida, kama ilivyokusudiwa awali.
Akizungumza mara baada
ya kukagua karakana Kuu za TAZARA jijini Dar es Salaam, Eng. Kasekenya amesema
ni wakati sasa kwa kila mwenye dhamana katika TAZARA kufanya kazi kwa
kuzingatia maono ya waasisi wa reli hiyo.
“…Tunao mzigo wa
kutosha wa kusafirisha kwa reli ya TAZARA hivyo hakikisheni mnakuja na mkakati
wa kibiashara utakaowezesha kuwa na vichwa vya treni na mabehewa yanayokidhi
mahitaji ya dunia ya sasa,” amesisitiza Eng. Kasekenya.
Amezungumzia umuhimu wa
karakana zote zilizopo kufanya kazi kikamilifu ili kupunguza msongamano wa
mabehewa na vichwa vya treni vinavyotakiwa kukarabatiwa.
Aidha ameitaka
menejimenti ya TAZARA kushirikiana na wafanyakazi katika hatua zote ili
kuongeza ari ya kufanya kazi pamoja na kutoa huduma zenye tija na kuvutia wasafirishaji
na abiria.
Naye Naibu Mkurugenzi
wa TAZARA, Eng. Christopher Shiganza amemhakikishia Naibu Waziri Kasekenya,
kuwa TAZARA wamejipanga kuhakikisha wanapata vichwa vya treni na mabehewa ya
kisasa ili kuongeza tija katika huduma hiyo.
Ameiomba Serikali kuboresha
sheria ya TAZARA ili kuimarisha umoja baina ya nchi wanachama na kuleta tija na
ufanisi mkubwa katika huduma za uchukuzi.
Reli ya TAZARA inayoanzia
Dar es Salaam, (Tanzania) hadi Kapirimposhi (Zambia), ilijengwa mwaka 1970 hadi
1975 kwa ushirikiano wa mataifa ya Tanzania na Zambia na imekuwa kichocheo
kikubwa cha maendeleo na udugu kati ya mataifa hayo mawili, ikiwa ni juhudi za
waasisi wa mataifa hayo Mwl. Julias Nyerere na Mzee Keneth Kaunda.
Imetolewa na Kitengo
cha Habari na Mawasiliano Serikalini, Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi.

No comments:
Post a Comment