Majaliwa ameyasema hayo baada ya kutembelea na kukagua hatua za ujenzi wa barabara ya mchepuo aliyoagiza ijengwe na TANROADS mnamo tarehe 04 Machi, 2020 ili kuondokana na msongamano wa magari yaliyokwama kwa muda wa takribani siku tano na kuridhishwa na kasi ya ujenzi wake.
"Nimepita mara ya pili kukagua hatua za ujenzi na nimeridhika kuona maendeleo yake kwani barabara hii ya mchepuo imeondoa foleni kubwa iliyokuwepo", amesema Waziri Mkuu Majaliwa.
Aidha, amewasihi mameneja wa TANROADS kuhakikisha wanakagua vipenyo vya madaraja yote hususani ya muda mrefu kuona kama ukubwa wake unaruhusu maji kupenya kwa urahisi hasa vipindi hivi vya mvua nyingi.
Majaliwa, ameitaka Wizara na TANROADS kuhakikisha fedha zinazotengwa kwa ajili ya matengenezo zinatumika kikamilifu ili kuboresha mawasiliano katika barabara kuu na kuhakikisha zinapitika majira yote ya mwaka.
Waziri Mkuu huyo ametoa wito kwa wananchi wote nchini kuwa wavumilivu katika maeneo yaliyopata athari za mvua hasa katika barabara na madaraja wakati Serikali inafanya utaratibu wa ukarabati wa miundombinu hiyo pindi mvua zitakapokamilika.
"Tunaelewa mvua zinanyesha hivyo nawaasa watanzania kuwa watulivu wakati kazi ya ukarabati zinafanyika kwa dharura kwanza hadi hapo hizi mvua zitakapoisha", amesisitiza Waziri Mkuu Majaliwa.
Awali akitoa taarifa ya ujenzi wa kalvati la zege katika eneo la Kiyegeya, Mtendaji Mkuu wa TANROADS, Mhandisi Patrick Mfugale, amemueleza Waziri Mkuu kuwa ujenzi wa awali waliweka makalvati ya chuma yenye urefu wa mita 12 kila moja kwa ajili ya dharura ambao uliwezesha magari kupita njia moja.
Mfugale amesema kazi inayoendelea hivi sasa ni ya kujenga kitako kitakachojengewa na kuunganishwa na kalvati la awali ili kuwezesha magari mawili kupita kwa pamoja.
"Hivi sasa magari yanayotoka njia ya Morogoro wanapita katika njia ya awali na yanayotoka Dodoma wanapita njia ya mchepuo ili kuruhusu ujenzi kuendelea" amefafanua Mhandisi Mfugale.
Ameongeza kuwa kazi hiyo ya ujenzi inatarajia kumalizika baada ya wiki mbili ili magari yaweze kutumia njia ya awali wakati wanaendelea na ujenzi wa tabaka la lami.
Imetolewa na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini,
Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
No comments:
Post a Comment