SAMIA AZITAKA NCHI WANACHAMA AU KUTOA MICHANGO - THE HABARII

THE HABARII

HABARI | MATUKIO | MICHEZO.


ASAS GROUP

Habari Mpya


Monday, 27 August 2018

SAMIA AZITAKA NCHI WANACHAMA AU KUTOA MICHANGO

Makamu wa Rais, Samia Suluhu Hassan.

Na Ahmed Mahmoud Arusha
MAKAMU wa Rais, Samia Suluhu Hassan ameziomba nchi wanachama wa umoja wa Afrika (AU) kutoa michango yao katika jumuiya hiyo kusudi kuziwezesha taasisi zake kufanya kazi kwa ufanisi.
Makamu huyo wa Rais ameyasema hayo leo Agost 27,Jijini Arusha baada ya kuapishwa kwa majaji wapya watatu wa mahakama ya Afrika ya haki za binadamu na watu (AFCHPR). Walioapishwa ni pamoja na Jaji Imani  Aboud kutoka Tanzania, Stella Anukam kutoka Nigeria na Jaji Blaise Tchikaya  wa Congo Brazzaville.
Samia amesema michango ya nchi wanachama ndiyo itawezesha mahakama hiyo kufanyakazi nzuri zaidi.
Miongoni mwa taasisi hizo za AU ni mahakama ya Afrika ya haki za binaadamu na watu (AFCHPR), yenye makao makuu jijini Arusha, inayodaiwa kukabiliwa na tatizo la rasilimali fedha ili kutimiza majukumu yake kwa wakati.
“Tujitahidi kukamilisha michango yetu ili mahakama hii ipate fedha, kama hawapati fedha za kutosha hawawezi kutekeleza vyema majukumu yao,” amesema Samia.
Amesema nchi nyingi za Afrika ziliridhia kuanzishwa kwa mahakama hiyo, hivyo zina wajibu wa kutoa michango yao AU kusudi mahakama ipate pia fedha badala ya kutegemea wafadhili.
Hata hivyo, amesema Serikali ya Tanzania inaunga mkono, mahakama hiyo na itaendelea kuipa ushirikiano wa hali na mali.
Amewapongeza majaji wapya waliochanguliwa ambao sasa wanaifanya mahakama hiyo, kuwa na majaji wanawake sita kati ya kumi na moja walipo.
“Ninawapongeza wanawake waliokabidhiwa nafasi kubwa katika mahakama hii, ninaimani kubwa kuwa watasaidia kuendesha haraka kesi na kutoa haki kwa watu wenye kesi zitakazofikishwa mbele yao,” amesema Suluhu.
Akizungumza baada ya kuapishwa,  Jaji Imani Aboud ameishukuru Serikali ya Tanzania kwa kumuunga mkono na amesema  atahakikisha anashirikiana na majaji wengine, ili haki itendeke bila woga wala upendeleo.
Amesema ushindi wake katika uchaguzi uliofanyika Mauritius unaonyesha jinsi umoja wa Afrika ulivyo na imani kubwa na Tanzania katika masuala ya haki za binaadamu na watu.
Akizungumzia Tanzania kuongoza kati ya mataifa yanayopeleka kesi katika mahakama hiyo, Jaji Imani Aboud amesema inatokana na kufika kwa urahisi katika mahakama hiyo, tofauti na nchi nyingine na haamini kama inatokana na mahakama za ndani kutofanya vizuri.
Awali, rais wa mahakama hiyo, Jaji Sylvain Ore ameelezea kuridishwa kwake na ushirikiano wa Tanzania katika kazi za mahakama hiyo na kwa niaba ya majaji, ametoa pole kwa msiba wa dada wa Rais John Magufuli, Monica, aliyefariki wiki iliyopita katika Hospitali ya Bugando mkoani Mwanza na maziko yake kufanyika kijijini kwao Wilayani Chato.
Mahakama ya Afrika ya Haki za Binadaamu kwa sasa ina jumla ya majaji kumi na moja ambao huchaguliwa kutoka nchi wanachama za AU. Majaji hao wapya watatumikia nafasi zao kwa kipindi cha miaka sita.

No comments:

Post a Comment