WWF YATOA ELIMU NA VIFAA MAALUM KUKABILIANA NA TEMBO WAHARIBIFU NAMTUMBO - THE HABARII

ASAS GROUP

Habari Mpya


Thursday 7 October 2021

WWF YATOA ELIMU NA VIFAA MAALUM KUKABILIANA NA TEMBO WAHARIBIFU NAMTUMBO

 

Mnyama aina ya tembo ambao wamekuwa wanafanya uharibifu wa mazao ya wakulima sasa watadhibitiwa kwa kutumia vifaa maalum kuwarudisha kwenye maeneo yao ya asili.

SHIRIKA la kimataifa WWF limetoa elimu na vifaa kwa kukabiliana na tembo waharibifu katika vijiji vitano vilivyopo Halmashauri ya Namtumbo mkoani Ruvuma.

Akizungumza wakati anamkabidhi vifaa hivyo, Mkuu wa Wilaya ya Namtumbo, Mhifadhi na Melimishaji wa WWF Ally Thabiti Mbugi  amesema wametoa elimu ya kujikinga na wanyama waharibifu hususan tembo kwa wananchi ili kukabiliana na uharibifu bila kuleta madhara kwa wanyama.

Mbugi amesema licha ya elimu, WWF pia imetoa msaada wa  vifaa mbalimbali vitakavyotumika kama nyenzo ya kukabiliana na tembo waharibifu ambapo vifaa aina ya vilipuzi 400 vimetolewa kwa wilaya ya Namtumbo.

Amevitaja vifaa vingine kuwa ni magunia ya pilipili,vilipuzi kamba na vitambaa vya pamba ambavyo vinatumika katika utengenezaji wa wigo wa pilipili ambao unasaidia kuzuia tembo wasiharibu mashamba ya wananchi.

‘’Hivi sasa tunakaribia msimu wa kilimo hivyo tumetoa elimu na vifaa mapema kabla ya uharibifu kufanyika, hata hivyo katika Mkoa wa Ruvuma tutatoa vilipuzi 800 katika wilaya za Namtumbo na Tunduru ambapo kuna uharibifu wa mazao unaofanywa na tembo, pia tumetoa mbegu za pilipili ili wananchi mwakani wasipate tabu,’’ alisema.

Akizungumza  mara baada ya kupokea  vifaa hivyo Mkuu wa Wilaya ya Namtumbo Dkt. Julius Ningu amewapongeza na kuwashukuru WWF kwa msaada huo kutokana na ukweli kuwa Namtumbo imeathirika na wanyamapori waharibifu wa mazao.

"Ukiangalia mkulima mtaji wake ni nguvu zake mwenyewe,na anafanya kilimo cha msimu, hivyo wanyama wanapoharibu mazao ni pigo kwake,’’alisisitiza.

Amesema msaada uliotolewa na WWF serikali na wananchi wanauthamini na wataifanyia kazi iliyokusudiwa na kwamba serikali itashirikiana na wananchi kuhakikisha wanyama waharibifu wanarejeshwa kwenye maeneo yao ya asili.

Amesema ameshukuru elimu na msaada huo kutekelezwa kabla ya msimu wa kilimo hivyo inatoa nafasi kwa serikali kuwaandaa wananchi  pamoja na namna ya kuvitumia vifaa vilivyoletwa ili vitumike kwa tija.

Imeandikwa na Albano Midelo

Afisa Habari Mkoa wa Ruvuma


No comments:

Post a Comment