MARUFUKU WAGANGA WA JADI KUPOKEA WAGONJWA WASIO NA RIPOTI ZA HOSPITALI - THE HABARII

ASAS GROUP

Habari Mpya


Thursday 16 April 2020

MARUFUKU WAGANGA WA JADI KUPOKEA WAGONJWA WASIO NA RIPOTI ZA HOSPITALI

Mkuu wa Mkoa wa Songwe Brig. Jen. Nicodemus Mwangela akishiriki kikao cha kamati ya Amani Mkoa ambapo amemuagiza Mganga Mkuu wa Mkoa wa Songwe kuhakikisha anatoa elimu ya tahadhari ya Corona katika nyumba zote za Ibada.

Mwenyekiti wa Kamati ya Amani Mkoa wa Songwe Sheikh Hussein Issa akizungumza na wajumbe wa kamati hiyo ambapo wamekubaliana kutoruhusu watoto katika nyumba za ibada ikiwa ni hatua mojawapo ya tahadhari zaidi juu ya ugojwa wa Corona.

KATIKA jitihada za kupambana na Ugonjwa wa Corona, Chifu wa Mkoa wa Songwe Mbeshena Nzunda ametoa marufuku kwa waganga wa jadi kupokea mgonjwa yeyote ambaye hana ripoti itakayo onyesha tatizo husika limeshindwa kutatuliwa hospitalini.

Chifu Nzunda amebainisha hayo katika kikao cha Kamati ya Amani ya Mkoa ilipokutana kujadiliana hatua zaidi za tahadhari zinazo paswa kuchukuliwa na Mkoa wa Songwe ili kupambana na ugonjwa wa Virusi vya Corona.

Amesema ili mgonjwa apate matibabu kwa mganga wa jadi anapaswa kuonyesha ripoti kuwa baada ya kutibiwa hospitalini hakupona na  wataalamu wa afya wathibitishe hilo pia waganga wa jadi wenye wateja wengi wanapaswa kuwahudumia kwa awamu ili kepusha msongamano.

Chifu Nzunda ameeleza kuwa waganga wa jadi wanatakiwa nao kuchukua tahadhari za Ugonjwa wa Corona kwa kunawa mara kwa mara kwa maji tiririka na sabuni pia kuweka maji hayo kwa ajili ya wateja watakao wahudumia.

Ameogeza kwa kuwataka watumiaji wa pombe za kienyeji kuhakikisha hawachangii vyombo vya kunywea pombe kama ilivyo zoeleka bali kila mmoja awe na chombo chake pia wauzaji  pombe hizo wachukue tahadhari kwa kuweka  maji ya kunawa pia kupunguza misongamano.

Mwenyekiti wa Kamati ya Amani Mkoa wa Songwe Sheikh Hussein Issa amesema kamati hiyo imekubaliana kuchukua baadhi ya hatua ikiwa ni kuongeza tahadhari Zaidi ya Ugonjwa wa Corona huku Uongozi wa Mkoa ukipongezwa kwa jitihada zilizochukuliwa hadi sasa hakuna mgonjwa wa Corona.

Sheikh Issa amesema kuanzia sasa watoto wasiruhusiwe kushiriki katika nyumba zozote za ibada ili kuwaondoa katika hatari ya maambukizi ya Corona pia wazazi wahakikishe watoto wanabaki majumbani.

Ameongeza kuwa nyumba zote za ibada zisiruhusu waumini wengi kujaa bali waingie wachache na wakae mbalimbali bil kusongamana pia maji tiririka ya kunawa na sabuni au vitakasa mikono  viwekwe ndani na nje ya nyumba hizo za Ibada.

Sheikh Issa amesema viongozi wote wa dini mbalimbali wanapaswa kuchukua tahadhari juu ya Ugonjwa wa Corona kwa kufuata maelekezo ya Serikali pia wasiache kumuomba Mungu ili ugonjwa wa Corona usilete maafa katika Nchi ya Tanzania.

Mkuu wa Mkoa wa Songwe Brig. Jen. Nicodemus Mwangela ameipongeza kamati hiyo kwa hatua hizo za tahadhari ya Corona huku akimuagiza Mganga Mkuu wa Mkoa wa Songwe kuhakikisha anatoa elimu ya tahadhari ya Corona katika nyumba zote za Ibada.

No comments:

Post a Comment